Nabi Amfungia Kazi Ninja
KATIKA kuhakikisha anaisuka vema safu ya ulinzi, Kocha Mkuu wa Yanga, raia wa Tunisia, Nasreddine Nabi, amemfungia kazi beki jihad, Abdallah Shaibu ‘Ninja’ kwa kumpa mbinu za kuwadhibiti mabeki wa wapinzani wao, Simba.
Timu hizo zinatarajiwa kuvaana Jumamosi hii saa kumi na moja jioni kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam.
Safu ya ushambuliaji ya Simba inatarajiwa kuongozwa na Denis Kibu, Chris Mugalu na John Bocco ambao huenda wakakutana na Ninja anayecheza soka la jihad na undava.
Mmoja wa mabosi kutoka ndani ya benchi la ufundi la Yanga, ameliambia Championi Ijumaa kuwa, kocha Nabi ameonekana akimpa mbinu na maelekezo ya jinsi ya kuwadhibiti washambuliaji katika mazoezi yake.
Juzi Jumanne beki huyo alianzishwa katika kikosi cha kwanza kilichocheza mchezo wa kirafiki dhidi ya DTB inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza aliyecheza pamoja na Yannick Bangala Litombo.
Aliongeza kuwa upo uwezekano mkubwa wa Ninja kuanza katika kikosi cha kwanza katika mchezo huo wa Ngao ya Jamii akicheza pamoja na Litombo.
“Kocha Nabi anaendelea kuboresha katika kila nafasi kwa kubadilisha wachezaji kwa lengo la kutengeneza kikosi imara kitakacholeta ushindani.
“Juzi (Jumanne) katika mchezo wa kirafiki dhidi ya DTB alionekana kuwabadilisha akina Mwamnyeto (Bakari) na Job (Dickson) kwa lengo la kuwaangalia Litombo na Ninja.
“Kikubwa anataka kuona safu ya ulinzi ikiwa imekamilika huku ikizuia hatari golini kwetu, hivyo kocha Nabi amevutiwa na Ninja, Litombo jinsi walivyocheza,” alisema bosi huyo.
Akizungumzia hilo, Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Frederick Mwakalebela, alisema: “Hilo ni suala la kiufundi, siyo sawa kulizungumzia nitakuwa kama ninaingilia majukumu ya kocha, hivyo ni vema tukamuachia kocha ambaye anajua mchezaji yupi yupo fiti kwa ajili ya mchezo huo.”
WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam