Nabi Ana Jambo lake Yanga SC
KOCHA Mkuu wa Yanga , raia wa Tunisia, Nasreddine Nabi anachokiangalia hivi sasa katika timu yake
ni matokeo mazuri ya ushindi pekee na siyo idadi ya mabao, aina ya soka.
Kauli hiyo aliitoa kabla ya mchezo wao wa Ligi Kuu Bara waliotarajiwa kucheza jana dhidi ya KMC FC
kwenye Uwanja wa Majimaji, Songea.
Yanga imekuwa ikipata matokeo kiduchu katika michezo yake miwili ya ligi ya ushindi wa bao 1-0 waliyoyapata dhidi ya Kagera Sugar nag EITA Gold.
Akizungumza na Championi Jumatano, Nabi alisema kuwa anachoangalia matokeo mazuri ya ushindi pekee ambayo ndiyo yatakayowawezesha wao kuubeba ubingwa wa ligi.
Nabi alisema kuwa kabla ya ligi kuanza aliomba miezi mitatu ya kuitengeneza timu itakayokuwa imara na itakayoleta ushindani, hivyo muda bado Wanayanga wasubirie muda ufike waone soka safi la kuvutia.
Aliongeza kuwa hivi sasa anaendelea kutengeneza muunganiko wa timu kwa kuanzia safu ya ulinzi na ushambuliaji ambayo hivi sasa ndiyo inayomuangusha kutokana na kufunga mabao kiduchu.
“Hakuna asiyefahamu uwezo wa kila mchezaji wangu, kikubwa wachezaji wangu wanahitaji kukaa pamoja kwa ajili ya kutengeneza muunganiko wa timu.
“Hivyo ni lazima nipate muda mzuri wa kutosha kuiandaa timu itakayocheza soka zuri la kuvutia lile ambalo mashabiki wanalitaka.“Pia kufunga idadi kubwa ya mabao, kwa hivi sasa ninachoangalia ni kuona timu inapata ushindi wa mabao yoyote ikiwemo bao 1-0 kwa lengo la kuongeza idadi ya pointi na siyo kufungwa iwe ndani au nje ya mkoa kwa lengo la kuchukua ubingwa msimu huu,” alisema Nabi.
Stori: Wilbert Molandi, Dar es Salaam