Nabi Anasa Siri za Wanigeria
TAYARI Kocha Mkuu wa Yanga, Nasreddine Nabi raia wa Tunisia, amefichua kuwa amezinasa mbinu za wapinzani wao, Rivers United ya Nigeria kabla ya mchezo wao wa Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya awali utakaochezwa wikiendi hii.
Kuelekea mchezo huo ambao utachezwa Uwanja wa Mkapa, Dar, Nabi amesema ameshafahamu mbinu wanazotumia Wanigeria hao.
Yanga chini ya Nabi, imejikita katika maandalizi ya mchezo huo katika kambi yao iliyopo Kigamboni, Dar licha ya kuwakosa baadhi ya mastaa wao waliokuwepo kwenye majukumu ya timu zao taifa.Kwa mujibu wa chanzo cha kuaminika kutoka ndani ya timu hiyo, kimeliambia Spoti Xtra kuwa:
“Mwalimu amekuwa bize katika kuwasoma wapinzani wetu, lakini bado kumekuwa na ugumu wa kupata video za mechi zao na kujua namna ambayo wanacheza.
“Licha ya hiyo, lakini amekuwa akiwasiliana na baadhi ya makocha anaofahamiana nao Nigeria ambao wamemueleza baadhi ya mambo ya umuhimu anayopaswa kuyafanyia kazi kabla ya mchezo huo.
“Kikubwa ambacho ameambiwa na amekuwa akikisisitiza kwenye mazoezi ni kwamba wapinzani wanatumia soka la nguvu lakini pia wanapenda kufanya mashambulizi ya kushtukiza kwa kutumia mipira mirefu jambo ambalo amekuwa nalo makini katika mazoezi ambayo timu inaendelea kufanya maana anachotaka ni kuona wanashinda si chini ya mabao mawili.
”Baada ya mchezo huo, timu hizo zinatarajiwa kurudiana Septemba 19, mwaka huu nchini Nigeria ambapo mshindi wa jumla atatinga hatua ya kwanza;
IBRAHIM MUSSA, DAR