The House of Favourite Newspapers

Nabi Ashikilia Faili la Farid Yanga

0

WAKATI tetesi zikisema kuwa kiungo mshambuliaji wa Yanga, Farid Mussa anaachwa mwishoni mwa msimu huu, lakini hatima ya nyota huyo amekabidhiwa Kocha Mkuu wa timu hiyo raia wa Tunisia, Nasreddine Nabi.

 

Farid hivi karibuni alirejea kikosini baada ya kupona majeraha yake yaliyomsababishia akae nje ya uwanja kwa muda mrefu.

 

Kiungo huyo tangu amerejea kikosini hapo, amekosa nafasi ya kuanza katika kikosi cha kwanza cha Nabi kinachoshiriki Ligi Kuu Bara na Kombe la FA.

 

Taarifa ambazo imezipata Spoti Xtra, Farid ni kati ya wachezaji ambao mikataba yao inatarajiwa kumalizika mwishoni mwa msimu huu.

 

Mtoa taarifa huyo alisema kuwa Farid alijiunga na timu hiyo kwa mkataba wa mwaka mmoja aliousaini katika msimu kutokana na malengo ya kutaka kwenda kucheza soka la kulipwa.

 

“Farid ni kati ya wachezaji ambao hatma yake inabaki mikononi mwa kocha Nabi ambaye yupo mazoezini akifuatilia kwa ukaribu kiwango chake.

 

Hatma yake rasmi itajulikana mwishoni mwa msimu huu ambao kocha atakabidhi ripoti ya mapendekezo ya usajili katika msimu ujao.

 

“Farid alijiunga na Yanga kwa mkataba wa mwaka mmoja, hivyo kama kocha akipendekeza abaki basi watamuongezea mkataba mwingine,” alisema mtoa taarifa huyo.

 

Akizungumzia mipango ya usajili katika kuelekea msimu ujao, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano na Usajili ya Yanga, Injinia Hersi Said, alisema kuwa: “Jukumu lote la usajili lipo mikononi mwa kocha wetu ambaye ndiye atakayepndekeza.”

Leave A Reply