The House of Favourite Newspapers

Nabi Atoa Maagizo Maalum Yanga

0

NASREDDINE Nabi, Kocha Mkuu wa Yanga, amewaambia wachezaji wake kuwa anahitaji watwae mataji mawili kwa msimu huu wa 2020/21 ili kufikia malengo ambayo walianza nayo mwanzo wa msimu.

 

Mataji hayo ni Kombe la Shirikisho la Azam ambapo tayari Yanga imetinga hatua ya nusu fainali baada ya ubao wa Uwanja wa Kambarage, Shinyanga kusoma Mwadui 0-2 Yanga, hivyo inatarajiwa kucheza na Biashara United.

 

Kwenye upande wa ligi, Yanga ipo nafasi ya pili ikiwa na pointi 61 baada ya kucheza mechi 29, ina mechi tano mkononi kukamilisha msimu huu.

 

Ofisa Mhamasishaji wa Yanga, Antonio Nugaz, alisema kuwa kocha huyo raia wa Tunisia aliongea na wachezaji na kuwaambia kwamba bado wana kazi ya kufanya kutimiza malengo ya msimu huu.

 

“Nabi ameongea na wachezaji na kuwaambia kwamba bado kazi inaendelea na anahitaji kuona wanafanikisha lengo la kufanya vizuri kwenye Kombe la Shirikisho pamoja na ligi kwani bado mapambano yanaendelea mpaka mwisho,” alisema Nugaz.

 

Makombe yote mawili ambayo wanapigia hesabu Yanga yapo mikononi mwa watani zao wa jadi, Simba ambao nao walibainisha kwamba wanayahitaji msimu huu.

 

Wakongwe hao wa soka Tanzania, huenda wakakutana kwenye fainali ya Kombe la Shirikisho la Azam endapo kila mmoja atashinda mechi yake ya nusu fainali. Simba ikicheza dhidi ya Azam na Yanga dhidi ya Biashara.

Leave A Reply