The House of Favourite Newspapers

Nabi Kuandika Historia kwa Wanigeria

0


KUELEKEA mchezo wa marudiano wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Rivers United ya Nigeria, Kocha Mkuu wa Yanga, Nasreddine Nabi anaweza kuandika historia ya kuwa kocha wa kwanza kuifunga Rivers United katika uwanja wao wa nyumbani wa Yakubu Gowon, tangu mwaka huu wa 2021 uanze.

 

Jumapili iliyopita kwenye mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika uliopigwa Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar, Rivers United waliibuka na ushindi wa bao 1-0, ambapo sasa Yanga wanajiandaa na mchezo wa marudiano utakaofanyika Septemba 19, nchini Nigeria.

 

Wakiwa katika uwanja wao wa nyumbani, Rivers United wamekuwa na takwimu nzuri wakiwa hawajapoteza mchezo wowote tangu kuanza kwa mwaka huu wa 2021 ambapo katika michezo 10 iliyopita, wameshinda mechi saba na kutoa sare mechi tatu, huku wakifunga mabao 17 na kuruhusu mabao matano pekee.

 

Akizungumza mara baada ya mchezo uliopita, Nabi alisema: “Tulifanya makosa kadhaa kwenye mchezo dhidi ya Rivers na kuruhusu kupoteza mchezo huo, lakini bado tunayo nafasi ya kufanya vizuri katika mchezo wa marudiano, hivyo tutarekebisha makosa yetu, na kupambana kushinda mchezo wa marudiano kule Nigeria na kufuzu hatua inayofuata.”

 

JOEL THOMAS, Dar es Salaam

Leave A Reply