The House of Favourite Newspapers

Nabi: Sababu ya Kiwango cha Fei Toto ni Hii

0

KOCHA Mkuu wa Yanga raia wa Tunisia, Nasreddine Nabi ametaja siri ya kiungo wake mchezeshaji Feisal Salum ‘Fei Toto’ ya kung’aa katika msimu huu.

Kauli hiyo ameitoa ikiwa timu hiyo imecheza michezo mitatu ya Ligi Kuu Bara ambayo yote wameshinda dhidi ya Kagera Sugar, Geita Gold na KMC FC.

Fei Toto ameonekana kuanza vizuri msimu huu kwa kufunga mabao mawili na asisti moja katika michezo mitatu aliyoicheza ya ligi.

Akizungumza na Championi Jumatatu, kwa niaba ya Nabi, Kocha msaidizi wa timu hiyo Mrundi, Cedric Kaze alisema kuwa siri ya kiungo huyo kuonekana bora kutokana kupunguziwa majukumu ya uwanjani.

Kaze alisema kuwa Fei Toto amewaachia kazi ya kukaba viungo wapya wakongwe Mganda Khalid Aucho na Mkongomani, Yannick Litombo Bangala.

Aliongeza kuwa jukumu lake ni kuchezesha timu na kumpigia pasi nzuri za mabao mshambuliaji Fiston Mayele anayecheza naye pacha katika kikosi cha kwanza.

“Fei Toto anaonekana akicheza vizuri na bora kutokana na uwepo wa viungo wakabaji Litombo na Aucho wanafanya majukumu ya kupunguza mashambulizi kwa wachezaji wa timu pinzani.

“Uwepo wa Aucho, Litombo unasaidia timu kucheza kwa kuelewana huku wakianzisha mashambulizi kwa kupitia katikati.

“Majukumu hayo awali alikuwa anayafanya Fei Toto aliyepewa majukumu ya kuchezesha timu na kupiga pasi za mwisho huku akiwa huru kuzunguka uwanja mzima,”alisema Kaze.

WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam

Leave A Reply