Nahodha AS Vita: Simba Hii Itatinga Nusu Fainali Caf
NAHODHA wa Klabu ya AS Vita kutoka DR Congo, Jeremy Mumberem, ameitabiria Simba kufanya vizuri kwa kusonga mbele dhidi ya wapinzani wao Kaizer Chiefs ya Afrika Kusini katika hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Simba katika hatua ya makundi ilipangwa kundi moja na AS Vita ambapo ilifanikiwa kupata ushindi katika michezo yote miwili ya nyumbani na ugenini waliyokutana.
Akizungumza na Championi Jumatatu, Mumbere alisema kuwa anaiona Simba ikiwatoa Kaizer Chiefs katika hatua ya robo fainali na kutinga nusu fainali kutokana na Simba kuwa na kikosi ambacho kina malengo makubwa ya kusonga mbele huku kikiwa kimeungana vizuri jambo ambalo ni silaha kubwa kwao na ya mafanikio.
“Simba imeungana vizuri sana, wachezaji wao wanafurahia kuwa sehemu ya kikosi cha Simba, wanafurahia kucheza mpira, aina yao ya kucheza inavutia na ina watu wa kuwapatia matokeo hata katika mazingira magumu.
“Kaizer Chiefs sio kwamba ni timu mbovu, hapana, ni timu nzuri ambayo ina kila kitu, wapo vizuri kiuchumi na wana wachezaji wenye majina makubwa na wakongwe lakini hawajakuwa na kipindi kizuri, matokeo yao yamekuwa ya kupanda na kushuka, ndio maana nawapa zaidi nafasi Simba ya kutinga nusu fainali kuliko wao,” alisema nahodha huyo.
MARCO MZUMBE,
Dar es Salaam