The House of Favourite Newspapers

Naibu Spika anusurika kifo baada ya kupata ajali jana

0
Naibu Spika Dk. Tulia Mwansasu.
NAIBU Spika Dk. Tulia Mwansasu, amepata ajali mkoani Mbeya alikokwenda kwa ajili ya mapumziko. Kwa mujibu wa Mkuu wa Wilaya ya Rungwe, Zainab Mbussi, Dk. Tulia alipata ajali hiyo jana wakati akitokea Mbeya mjini akielekea Kyela.
Mkuu wa wilaya alisema ajali hiyo ilitokea katika eneo la Shule ya Sekondari ya Kipoke iliyoko wilayani humo.
Alisema maelezo ya askari wa usalama barabarani, yanaeleza kuwa chanzo cha ajali hiyo ni gari dogo lililoelezwa kuwa liliibeba familia ya mtu aliyetajwa kwa jina moja la Chacha, lililokuwa likitokea Kyela kwenda Mbeya, lilipojaribu kulipita lori na kukutana na gari la Naibu Spika.
Zainab alisema Dk. Tulia, mdogo wake pamoja na mlinzi wake waliokuwa kwenye gari lake wako salama ingawa gari hilo limeharibika vibaya sehemu za mbele.
Aidha, alisema baadhi ya abiria waliokuwa kwenye gari la Chacha wakiwemo wanawe wawili walipata majeraha na walipelekwa katika hospitali ya Mission Igogo, Kiwira.
Awali mapema jana, Dk. Tulia, alitoa msaada wa sh. milioni tano, ili kulifanyia ukarabati bweni  la Mapinduzi, ambalo alikuwa analala wakati anasoma Shule ya Sekondari ya Wasichana Loleza, iliyopo jijini Mbeya.
 Dk. Tulia ambaye alisoma shuleni hapo kuanzia kidato cha kwanza hadi cha nne, mwaka 1991 hadi 1994, pia alitoa msaada wa magunia mawili ya mchele kwa ajili ya chakula kwa wanafunzi.
Akizungumza na walimu na wanafunzi, Dk.Tulia alisema ametajiwa changamoto nyingi, zinazoikabili shule hiyo na kuwa amzichukua na kuahidi kutafuta wadau atakaoshirikiana nao ili waweze kusaidia kuzitatua.
Dk. Tulia alisema ameguswa na uchakavu wa mabweni, ambapo alipata fursa ya kuonyeshwa yakiwemo mawili aliyokuwa analala akiwa shuleni hapo, ambayo ni Kibo linaloendelea kutumika hadi sasa na lile la Mapinduzi ambalo kwa sasa halitumiki.
“Kwenye bweni nililokuwa nikikaa nimepita mwenyewe. Naahidi kushughulika na lile bweni la Mapinduzi ndilo lililo kwenye hali mbaya zaidi kiasi cha kushindwa kuendelea kutumika,” alisema Dk.Tulia.
Dk.Tulia alitoa magunia mawili ya mchele, kwa ajili ya chakula kwa wanafunzi shuleni hapo na aliwachekesha wanafunzi pale aliposema katika mambo ambayo hayajabadirika shuleni hapo ni ratiba ya kula wali mara mbili kwa wiki.
“Kwa sababu mimi dada yao nimewatembelea leo, na waswahili wanao msemo ‘mgeni njoo mwenyeji apone’, basi mimi nitawaletea magunia mawili ya mchele ili angalau kwa hizi wiki wanafunzi wawe wananikumbuka,” alisema Dk.Tulia.
Naye, mbunge wa Songwe, Philip Mulugo, alimuunga mkono Dk.Tulia kwa kuchangia sh. milioni moja, kwa ajili ya kusaidia ukarabati wa bweni hilo la Mapinduzi.
Viongozi mbalimbali wa Chama na serikali, wakiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Munasa Nyerembe, walikuwepo katika ziara hiyo na Naibu Spika kutembelea shule hiyo ambayo hivi sasa inachukua wanafunzi wa kidato cha tano na sita tu.
Leave A Reply