Naj: Napenda Kukumbatiwa
MY Style kama kawaida tunakutana na mastaa mbalimbali Bongo na kupiga nao stori mbalimbali kuhusu ‘life style’ yao mbali na kazi wanazofanya.
Leo tupo na msanii wa muziki wa Bongo Fleva, Najma Dattan ‘Naj’ ambaye pia ni mpenzi wa msanii wa Bongo Fleva; Baraka Andrew ‘Baraka The Prince’. Amefunguka mambo mengi usiyoyajua, ungana nami kwa mahojiano zaidi:
My Style: Mambo Naj! Kitambo sana sijakuona, ulipotelea wapi?
Naj: Poa, nashukuru nimerudi salama. Nilikuwa London ambako ndiko huwa naenda na kurudi kwa sababu wazazi wangu pia wapo huko.
My Style: Sawa, hivi jambo la kwanza kufanya pindi unapoamka kitandani ni nini?
Naj: Nikiamka jambo la kwanza kufanya, lazima nichukue simu kisha nimpigie mpenzi wangu, kwa sababu London na Tanzania kumetofautiana saa tatu, kwa hiyo mimi nikiamka yeye anakuwa ameshaamka saa nyingi kabla. Hivyo, lazima nitakutana na missed call au message, hivyo nakuwa na respond (anajibu) hivyo.
My Style: Baada ya hapo huwa unafanya vitu gani?
Naj: Baada ya hapo naingia jikoni kutengeneza chai, nikimaliza naandaa kabisa, kisha ndipo naenda bafuni kuoga. Nikimaliza, sasa narudi tena mezani kwa ajili ya kunywa chai yangu.
My Style: Umesema ukiamka jambo la kwanza ni kumpigia mpenzi wako, natamani kujua kwa siku huwa unampigia simu mara ngapi?
Naj: Inategemea, kama niko bize sana siku hiyo basi naweza nikamtafuta mara nne, lakini kama niko free atakoma; yaani atajuta na asipopokea simu yangu, ndipo nitapiga sana siku hiyo.
My Style: Inaweza ikapita siku haujamtafuta?
Naj: Hapana, siwezi labda kama siku hiyo tumegombana, lakini hata kama ikiwa hivyo, mara nyingi mimi ndio huwa najishusha na kuanza kumtafuta.
My Style: Baraka ni mwanaume wa aina gani tangu umeanza kuwa naye? Ni jambo gani ambalo huwa anakushauri ambalo mpaka sasa unaona umuhimu wake?
Naj: Well, Baraka ni mwanaume wa tofauti sana na wanaume wengine ambao nimewahi kukutana nao. Anajali, anathamini na kupenda kweli, kitu ambacho huwa ananishauri ni kuhusu kutokuwa na marafiki wengi ambao hawana mchango wowote kwangu, hivyo kwa sasa naweza kusema nimeshapunguza marafiki zangu wengi sana na kubaki nao wachache, kwa sababu pia maisha yameshabadilika na ratiba zetu zinatofautiana na hata malengo yetu pia hayafanani. Lakini mbali na yote, nimeamua kubadilisha life style yangu yote ya zamani kama kujirusha kwenye kumbi za starehe na vitu kama hivyo.
My Style: Umbali wenu huwa unakuathiri chochote?
Naj: Ndio unaniathiri, kwa sababu huwa nakumbuka usiku tunavyokuwa tumelala huwa ananikumbatia sana, halafu na mimi kiukweli napenda sana kukumbatiwa. Hivyo, nikiwaga naye mbali napata shida kwa kweli, kwa sababu hata tukiwa tumegombana, ikifika tu usiku nitatafuta njia yoyote ile ili tuanze kuelewana kwa sababu sitaweza kulala naye halafu asinikumbatie.
My Style: Mara kadhaa Baraka amekuwa akikusifia kwamba, wewe ni mwanamke muelewa pamoja na kwamba amekuwa akikukosea lakini mara nyingi umekuwa ukijishusha na kumshauri mambo mema. Pamoja na kupigania penzi lenu mpaka leo, una ushauri gani kwa wanawake ambao wamekuwa wakikaa muda mfupi kwenye uhusiano wao kwa kukosa uvumilivu?
Naj: Jambo kubwa ni kuvumiliana na kuangalia wapi umetoka na wapi unakwenda kwa sababu kila mwanaume ana mapungufu yake, hivyo huwezi kubadilisha wanaume kila siku, utaonekana malaya na kama mnavyojua thamani ya mwanamke ipo kwenye mwili wako, hivyo wao wenyewe wajitambue.
My Style: Ukiwa na msongo wa mawazo, huwa unapenda kufanya nini?
Naj: Nikiwa na mawazo huwa napenda kukaa chumbani kwangu kisha naanza kuangalia tamthiliya, Chanel za wanyama pamoja na kuangalia reality shows kwa sababu hivyo ndio vitu ambavyo huwa vinanipotezea mawazo.
My Style: Ukitulia tu nyumbani na mpenzi wako, huwa unapenda kufanya nini?
Naj: Tukiwa nyumbani, mara nyingi huwa napenda sana kupika kwa sababu mpenzi wangu anapenda sana kula. Muda wote nakuwa napika, yaani asubuhi, mchana mpaka jioni.
My Style: Anapendelea zaidi chakula gani?
Naj: Anapenda sana maharage na chapati au maharage na wali.
My Style: Kitu gani ambacho unakipenda sana toka kwa mpenzi wako?
Naj: Vingi sana, lakini kikubwa napenda sana mashavu yake na lips. Yaani ana mashavu mazuri sana ya kukiss.
My Style: Unapenda rangi gani ya nguo?
Naj: Rangi ninayoipenda sana ni kijani.
My Style: Kwa nini wewe huna tattoo mwilini mwako kama ilivyo kwa wasanii wengine wa kike?
Naj: Sina kwa sababu familia yangu inajua sana dini, sasa sitaki muziki au ustaa nilionao uwafanye wazazi wangu wajute kwa kufanya vitu ambavyo vinakuja kutuathiri sana baadaye.
MAKALA: MEMORISE RICHARD