NAMITE: Ngozi Yangu Nyeupe, Damu Yangu ya Kitanzania
MWANAMUZIKI mdogo, Namite Selvaggi, ambaye makazi yake ni nchini Italia, amesema kuwa siku zote anajivunia kuwa na damu ya Tanzania japokuwa rangi yake inaonekana ya Kizungu, na ndiyo maana kila wimbo anaoimba anauimba kwa lugha ya Kiswahili na anaipenda lugha hiyo.
Akizungumza na Showbiz, Namite ambaye ameshatoa nyimbo takribani tano ambazo ni Utalii, Mazingira, Tanzania na nyingine nyingi, amesema kuwa kitu kikubwa alichokuwa akifanya ni kujifunza Kiswahili na mwalimu wake mkubwa alikuwa mama yake ambaye ni Mtanzania ambapo baba yake ni raia wa Italia.
“Mimi usinione mweupe lakini ukweli ni kwamba damu yangu ni ya Kitanzania, napenda sana nchi yangu, na ndiyo maana kila wimbo ninaoimba naimba Kiswahili kwa sababu naamini moyo wangu wote unaipenda Tanzania,” alisema Namite ambaye hivi karibuni atatoa wimbo wake wa ‘Utamaduni’.
Na Imelda Mtema