Namungo Yachekelea Waangola Kuletwa Dar
UONGOZI wa Klabu ya Namungo, umesema kuwa maamuzi ya Kamati Maalum ya Shirikisho la Soka Afrika (CAF), kupanga michezo yote miwili ya hatua ya 32 bora kati ya timu hiyo dhidi ya Clube Desportivo 1º de Agosto ya Angola ipigwe jijini Dar, ni faida kubwa kwao.
Hatua hiyo imekuja baada ya Namungo kurejea nchini wakitokea Angola ambapo walikumbana na matukio mengi yaliyofanya mchezo wao uliopangwa kuchezwa wikiendi iliyopita kuahirishwa na CAF.
Uamuzi huo wa Kamati Maalum ya CAF iliyokuwa ikishughulikia sakata hilo, umekuja baada ya kubainika kuwa si wenyeji wa mchezo huo wa awali wala Namungo, iliyohusika moja kwa moja kukwamisha mechi hiyo, hivyo kuamuru mechi zote mbili kuchezwa angalau ndani ya saa 72, na ziwe zimechezwa kufikia Februari 26.
Agosto watakuwa mwenyeji wa mechi ya kwanza, huku Namungo wao wakiwa wenyeji kwenye mchezo wa pili.
Akizungumza na Spoti Xtra, Ofisa Habari wa Namungo, Kindamba Namlia, alisema: “Maamuzi yaliyotolewa na Shirikisho la Soka Afrika tumeyapokea, na hatuwezi kuyalalamikia kwa sababu wao wamefanya tathimini ya kile ambacho kilitokea Angola na kuja na maamuzi hayo.
“Jambo zuri ni kwamba wakati huu sisi tutakuwa nyumbani, kimazingira hii ni faida kwetu na kikosi tayari kimeanza mazoezi tangu Jumanne kuelekea mchezo wetu wa kwanza ambao tutacheza Februari 21, hatuna majeruhi yoyote.”
JOEL THOMAS, Dar es Salaam