The House of Favourite Newspapers

Nandy, Zuchu Ndani Ya Mchuano Mkali AFRIMMA

0

WASANII wa kike wanaosumbua katika muziki wa Bongo Fleva, Faustina Charles ‘Nandy’ na Zuhura Kopa ‘Zuchu’ wapo kwenye mchuano mkali, kufuatia kuingia kwenye kinyang’anyiro cha kuwania Tuzo za AFRIMMA.

 

Wawili hao wanachuana kwenye kipengele cha Msanii Bora wa Kike Afrika Mashariki, ambapo kwenye mitandao ya kijamii, wameonekana kuwagawa mashabiki wa burudani Bongo.

 

Kuna ambao wanahamasisha kumpigia kura Zuchu, ambaye hana muda mrefu kwenye gemu, lakini wapo pia ambao wanampigia chapuo Nandy, wakisema uwezo wake ni mkubwa.“Aliyetangulia katangulia tu, Zuchu hamuwezi Nandy hata kwa dawa, niamini mimi,” alichangia mdau mmoja mtandaoni, huku wengine pia wakipinga kauli hiyo kwa kusema kutangulia sio kufika.

Mbali ya Zuchu na Nandy, kwenye kipengele hicho cha Msanii Bora wa kike, wapo pia wasanii mbalimbali ndani ya Afrika Mashariki akiwemo Nadia Mukami (Kenya), Tanasha Donna (Kenya), Maua Sama (Tanzania), Rosa Ree (Tanzania), Vimka (Uganda) na wengine wengi.

 

Mchuano huo unaonekana kuwa kabambe Bongo baina ya Nandy na Zuchu, kufuatia warembo hao kuachia nyimbo kali hivi karibuni, zinazoonekana kupendwa na kuwa na mashabiki wengi.

 

Nandy anatamba na kibao chake cha Acha Lizame alichomshirikisha Harmonize, huku Zuchu akitamba na kibao chake cha Nisamehe.Tuzo hizo zilizokuwa na vipengele mbalimbali, zinatarajiwa kutolewa Novemba 15, mwaka huu katika jiji la Dallas, Texas, Marekani.

Waandishi: Elizabeth Philimin na Mashauri Samwel (TUDARCo).

Leave A Reply