Nasreddine Nabi Achimba Mkwara Mzito
KOCHA Mkuu wa Yanga, Nasreddine Nabi, ameweka wazi kuwa amekiandaa kikosi chake kuibuka na
ushindi katika mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya KMC utakaopigwa keshokutwa Jumanne, licha ya ugumu wa wapinzani wao na mazingira ya uwanja ambayo wataenda kuchezea.
Mchezo huo wa raundi ya tatu, umepangwa kuchezwa Uwanja wa Majimaji uliopo Songea ambapo wenyeji ni KMC.
Akizungumza na Spoti Xtra, Kocha Nabi alisema: “Kikosi chetu kinaendelea vizuri na programu za
mazoezi ya kujiandaa na michezo ijayo ya Ligi Kuu Bara hususani dhidi ya KMC ambao tutacheza Oktoba 19, mwaka huu.
“Tunafurahi kuona idadi kubwa ya wachezaji waliokuwa kwenye vikosi vya timu za taifa wameripoti kambini kwa ajili ya kuendelea na programu za pamoja na wenzao, tunajua KMC ni timu ngumu na hata mazingira ya uwanja hayatakuwa rafiki.
“Lakini ni lazima tuhakikishe tunapata pointi tatu katika mchezo huo, ili kuendelea kujiweka katika nafasi nzuri ya kutimiza malengo ya kutwaa ubingwa msimu huu.”Leo Jumapili, kikosi cha Yanga kinatarajiwa kutoka Dar kuelekea Songea kwa ajili ya mchezo huo.
Yanga imeanza msimu vizuri kwa kushinda mechi mbili za ligi dhidi ya Kagera Sugar na Geita Gold, ikijikusanyia pointi sita.