Nchimbi Aumia Taifa Stars
KIKOSI cha Taifa Stars kikiwa kinaendelea na maandalizi ya mechi ya kirafiki dhidi ya Kenya na za kufuzu AFCON dhidi ya Libya na Equatorial Guinea, mazoezi ya jana asubuhi kilikosa huduma ya straika wake, Ditram Nchimbi.
Nchimbi alikosekana katika mazoezi hayo yaliyofanyika Uwanja wa Mkapa, Dar, baada ya kuumia nyama za paja.
Mwingine ambaye hakuwepo ni David Bryson.
Daktari wa Taifa Stars, Richard Yombo, alisema: “Wachezaji wawili wamepata majeraha ya nyama za paja ambao ni Ditram Nchimbi na David Bryson ndiyo maana hawapo mazoezini, lakini waliobaki wote ni wazima.
”Naye Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Kim Poulsen, alisema: “Tunashukuru Shirikisho kwa kutuwekea mechi mbili za maandalizi dhidi ya Kenya kabla ya kuvaana na Equatorial Guinea.
Leo (jana asubuhi) tumefanya mazoezi na wachezaji 23, wamekosekana wawili.“Kikubwa tumefanyia kazi kuanzia eneo la ulinzi, kiungo na ushambuliaji ili kupata matokeo mazuri katika michezo ya kufuzu.”
Taifa Stars ikiwa Kundi J, inashika nafasi ya tatu baada ya kukusanya pointi nne. Vinara ni Tunisia wenye kumi, huku Equatorial Guinea wakiwa na sita, wakati Libya wakishika nafasi ya mwisho kwa kuwa na pointi tatu.
STORI: LEEN ESSAU, Dar es Salaam