The House of Favourite Newspapers

NDONYA KWA WAMAKONDE ILIKUWA SILAHA YA KUJILINDA

WAMAKONDE na Wameto wa Msumbiji wanaishi katika Mkoa wa Cabo Delgado Kaskazini-Mashariki mwa nchi hiyo na Wamakonde wa Tanzania wanaishi zaidi katika wilaya zote za Mkoa wa Mtwara ila Masasi na Nanyumbu wapo kwa asilimia ndogo na huishi na wenyeji wao Wamakua na Wayao.

 

Wamakonde wamejipatia umaarufu mkubwa nchini Tanzania kutokana na kuwa na ukakamavu na shughuli za uchongaji wa vinyago. Tofauti kubwa kati ya Wamakonde wanaoishi Kusini mwa Mto Ruvuma (Msumbiji) na Kaskazini mwa Ruvuma (Tanzania) ni aina ya urembo wa ndonya. Wale wa Msumbiji wana ndonya ndogo juu ya midomo yao wakati wa Tanzania wana ndonya kubwa zaidi midomoni mwao.

 

Wamakonde huonekana kwa uzuri wao, wapo waliochanja sehemu za juu ya mdomo, masikio na uso. Inaaminika kuwa chanzo cha kuchanja, kutoboa midomo na kuweka ndonya ilikuwa kujilinda dhidi ya wafanyabiashara wa watumwa ambao walibeba watumwa kwenda kwenye mashamba huko Ulaya.

 

Ndonya na chanjo ziliwakasirisha sana wafanyabiashara wa Kiarabu kwa kuona kuwa watu hao hawapendezi. Wamakonde wengine wa Msumbiji waliamua kuchonga meno yao, ili kujilinda, kwamba mtu ambaye angeingia katika himaya yao akiwa hajachanja, hana ndonya na hajachonga meno, walimuona ni adui yao na kama ni mweusi, ni mpelelezi wa Waarabu ili wavamie kuwachukua kwenda utumwani.

 

Tabia hizi zikawa ni desturi na mila zao na zikawa kama urembo ndani ya kabila la Wamakonde. Baada ya kukomeshwa kwa biashara ya watumwa, mila hizi zilianza kutoweka na wengi wameachana nazo.

Comments are closed.