The House of Favourite Newspapers

NEMC: MAJI YATOKAYO MGODINI YANA SUMU

JANUARI 10 mwaka huu wataalamu wa Baraza la Usimamizi na Uhifadhi wa Mazingira nchini (NEMC) lililopo chini ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais – Mazingira na Muungano, January Makamba wametoa taarifa mjini hapa kuwa maji yaliyolalamikiwa na wananchi wa vijiji vya kuzunguka mgodi wa dhahabu wa North Mara yana sumu.

 

Ukweli huo ulitolewa na wataalam hao hivi karibuni kukiwa na wataalam wa kutoka katika Wizara za Maji na Umwagiliaji, Wizara ya Madini na ile ya mazingira walipokuwa na makatibu wakuu wa wizara hizo katika eneo la vijiji vya mgodi huo.

 

Makatibu wakuu hao na wataalam wake walifika katika vijiji vya mgodi huo na walitoa ukweli huo baada ya kumalizika upimaji wa sampuli za maji zilizokuwa zimechukuliwa na wataalam katika maeneo ya vyanzo mbalimbali vya maji yanayotumiwa na wakazi na mifugo yao kwa matumizi ya kunywa na kuoga.

 

Baada ya kutoa ukweli huo wakuu hao waliupatia muda wa miezi nane tangu siku hiyo kuhakikisha mgodi huo (ACACIA) unachimba bwawa lingine la kutunzia maji ya sumu kutokana na kwamba bwawa lililopo la Nyabirama limejaa na maji yanatiririkia katika makazi ya watu na kuingia katika visima na mito wanayoyatumia muda wote na mifugo yao hiyo.

Aidha, katika taarifa hiyo wataalam hao pia waliukosoa mgodi huo ulioanzisha bwawa lingine la Nyabigena bila kuzingatia sheria za uhifadhi wa sumu ambapo walisema watauadhibu mgodi huo.

Hatua ya kuchunguza maji hayo ilikuja baada ya Rais Dk John Pombe Magufuli kuagiza kupimwa maji yote ya vyanzo vinavyolalamikiwa muda mrefu bila kupatiwa ufumbuzi wake.

 

Baada ya agizo hilo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi ya Mazingira (NEMC), Dk Vedast Makota, alikuja Tarime na akasema wameanza kutekeleza agizo hilo kwa kuchukua sampuli katika maeneo yote ili kubaini kama zina madhara kwa viumbe hai au la.

 

Baadhi ya wafugaji ambao mifugo yao ilikufa kutokana na maji hayo ni pamoja na ya marehemu Mang’era Nyamboge Ntora, Daniel Ryoba Irondo ambaye ni mwenyekiti wa Kijiji cha Matongo na wafugaji wengine huku baadhi yao katika vijiji vya kuzunguka mgodi huo bado wanaugulia majumbani mwao wengine wakidaiwa kufa kutokana na madhara ya maji hayo.

Igenga Mtatiro, Mara

Comments are closed.