KIWANGO kinachoonyeshwa na Manchester City hivi sasa kimemfanya gwiji Phil Neville anyooshe mikono na kutamka: “Hawa jamaa hawatafungika msimu huu.
” Ni baada ya City kuichapa Leicester City 0-2 na kuwa na mwanzo mzuri zaidi wa Premier katika historia yao, wakiwa wameshinda mechi kumi mfululizo katika ligi hiyo.
Vijana hao wa kocha Pep Guardiola wamecheza mechi 12 na hawajapoteza mchezo wowote, wakiwa na sare moja tu. Wapo mbele ya msimamo kwa tofauti ya pointi nane. “Nadhani wanaweza kwenda msimu mzima bila kupoteza mechi. Wana ubora huo, na sioni ni kwa vipi timu inaweza kuwanyang’anya pointi,” alisema nyota huyo wa zamani wa Man United.