The House of Favourite Newspapers

Ngoma Fresh Azam, Chirwa Bado

Donald Ngoma (kushoto) akikabidhiwa mkataba mpya wa mwaka mmoja kuendelea kuitumikia timu hiyo.

AZAM FC imetangaza kumuongeza mkataba mshambuliaji wake, Donald Ngoma huku wakiwa bado kwenye mazungumzo na Obrey Chirwa ambaye inadaiwa amekuwa akisumbuasumbua kusaini.

 

Ngoma alijiunga na Azam FC mwanzoni mwa msimu huu kama mchezaji huru akitokea Yanga ambako alivunja mkataba wake. Chirwa yeye alijiunga na Azam dirisha dogo akitokea Nogoom FC ya Misri.

 

Ngoma ameongeza mkataba wa mwaka mmoja juzi utakaomfanya adumu kikosini humo mpaka mwaka 2020 na Chirwa yeye anaendelea na mazungumzo. Wachezaji wengine ambao wapo kwenye mazungumzo ya kuongeza mkataba mpya ni Mwadini Ally, Stephan Kingu na Abdallah Kheri.

 

Mratibu wa Azam FC, Philip Alando ameliambia Championi Jumamosi kuwa: “Tayari tumeshamsainisha mchezaji wetu Ngoma mkataba mwingine wa mwaka mmoja ambao unatarajiwa kuisha mwaka 2020 ikiwa ni zoezi linaloendelea hivi sasa la kuwaongezea mikataba wachezaji wanaotarajia kumaliza mikataba mwishoni mwa msimu huu.

 

“Zaezi hili linawahusu wale tu ambao wanamaliza mikataba na si wale wenye mikataba mirefu, tumeamua kufanya hivyo kwa kuwa hatuna mpango wa kumuacha mchezaji wetu hata mmoja mwishoni mwa msimu.

 

“Kwa upande wa Chirwa yeye zoezi bado halijakamilika, tunaendelea na mazungumzo naye, tutasubiria hadi mwishoni mwa msimu ndiyo tutajua juu ya kumuongezea mkataba mwingine kwa kuwa mkataba wake unaisha mwezi Julai, mwaka huu,” alisema Alando.

Stori na Khadija Mngwai, Dar es Salaam

 

View this post on Instagram

 

NGOMA AONGEZA MWAKA MMOJA AZAM FC MSHAMBULIAJI wa Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati Azam FC, Donald Ngoma, amesaini mkataba mpya wa mwaka mmoja kuendelea kuitumikia timu hiyo. Nyota huyo raia wa Zimbabwe, alijiunga Azam FC msimu huu Juni mwaka jana kwa mkataba wa mwaka mmoja uliokuwa unamalizika mwishoni mwa msimu huu, hivyo kwa kusaini kandarasi hiyo mpya ataendelea kubakia hadi Juni 2020. Ngoma, aliyekosa mechi za mwanzo wa ligi baada ya kuwa majeruhi wa muda mrefu, hadi sasa ni miongoni mwa wafungaji bora wa timu hiyo msimu huu, akiwa amefunga mabao tisa kwenye mashindano yote sawa na Obrey Chirwa, huku akiwa amechangia pasi nne za mabao. Mpaka sasa ameshiriki kwenye mafanikio ya Azam FC kutwaa taji la Mapinduzi Cup, akiwa amefunga mabao mawili na kutoa pasi moja ya mwisho kwenye michuano hiyo, huku kwenye ligi akiwa amefunga mabao saba. #ContractRenewal #Ngoma2020 #AzamFC #TimuBoraBidhaaBora #AfricanFrutiImenogaFresh #UhaiDrinkingWater #TradegentsTanzaniaLimited

A post shared by Azam Football Club🇹🇿 (@azamfcofficial) on

Comments are closed.