Ngoma Fresh Azam, Chirwa Bado
AZAM FC imetangaza kumuongeza mkataba mshambuliaji wake, Donald Ngoma huku wakiwa bado kwenye mazungumzo na Obrey Chirwa ambaye inadaiwa amekuwa akisumbuasumbua kusaini.
Ngoma alijiunga na Azam FC mwanzoni mwa msimu huu kama mchezaji huru akitokea Yanga ambako alivunja mkataba wake. Chirwa yeye alijiunga na Azam dirisha dogo akitokea Nogoom FC ya Misri.
Ngoma ameongeza mkataba wa mwaka mmoja juzi utakaomfanya adumu kikosini humo mpaka mwaka 2020 na Chirwa yeye anaendelea na mazungumzo. Wachezaji wengine ambao wapo kwenye mazungumzo ya kuongeza mkataba mpya ni Mwadini Ally, Stephan Kingu na Abdallah Kheri.
Mratibu wa Azam FC, Philip Alando ameliambia Championi Jumamosi kuwa: “Tayari tumeshamsainisha mchezaji wetu Ngoma mkataba mwingine wa mwaka mmoja ambao unatarajiwa kuisha mwaka 2020 ikiwa ni zoezi linaloendelea hivi sasa la kuwaongezea mikataba wachezaji wanaotarajia kumaliza mikataba mwishoni mwa msimu huu.
“Zaezi hili linawahusu wale tu ambao wanamaliza mikataba na si wale wenye mikataba mirefu, tumeamua kufanya hivyo kwa kuwa hatuna mpango wa kumuacha mchezaji wetu hata mmoja mwishoni mwa msimu.
“Kwa upande wa Chirwa yeye zoezi bado halijakamilika, tunaendelea na mazungumzo naye, tutasubiria hadi mwishoni mwa msimu ndiyo tutajua juu ya kumuongezea mkataba mwingine kwa kuwa mkataba wake unaisha mwezi Julai, mwaka huu,” alisema Alando.
Stori na Khadija Mngwai, Dar es Salaam
Comments are closed.