The House of Favourite Newspapers

Nilifanya Mapenzi na Maiti 20 Nitajirike-25

ILIPOISHIA

Nilihisi hisia zote, nilijua kwamba nilikuwa nafanya mapenzi na Majeed lakini cha kushangaza baada ya dakika kadhaa, nikashtuka kutoka usingizini, nilikuwa ndani ya chumba cha Majeed, sikuwa na nguo hata moja mwili mwangu, wakati najiuliza ni kitu gani kimetokea, nikasikia sauti moyoni mwangu ikiniambia “Umefanya mapenzi na jini kwa mara ya pili, umeingia kwenye mtego wake, kujinasua ni mpaka rehema yangu itakapokushukia.”

NIKASHTUKA.  

ENDELEA NAYO

Hiyo ilikuwa ni mara ya pili sauti hiyo kunijia kichwani, nilijiuliza sana kuhusu sauti hiyo lakini sikupata jibu lolote lile. Maneno iliyoniambia kwamba nilifanya mapenzi na jini yalinichanganya sana, nikabaki nikijiuliza kwamba je, huyu Majeed alikuwa jini au?

Sikuwa na jibu, nilitulia chumbani hapo huku nikiwa na hofu kubwa moyoni mwangu. Kilichonishangaza, nilifanya mapenzi kwenye ndoto sasa iweje kwenye uhalisia niwe nimechoka kana kwamba nilifanya mapenzi katika ulimwengu halisi?

“Inawezekanaje?” nilijiuliza.

Hata kabla sijapata jibu, mara mlango ukafunguliwa na Majeed kuingia ndani. Nilimwangalia machoni mwake, alionyesha tabasamu pana, alikuwa amekuja na chakula mpaka pale chini nilipokuwa.

Nilimwangalia kwa mshangao, yeye mwenye aliligundua hilo kwamba ilikuwaje mpaka niwe nimebdailika namna hiyo? Akanisogelea na kunishika bega.

“Kuna nini?” aliniuliza huku akiniangalia.

“Hivi nimefanya mapenzi na wewe?” niliuliza huku nami nikimwangalia.

“Hapana! Nilikwambia usubiri mpenzi.”
“Lakini kwa nini nipo hivi?”

“Upo vipi?”
“Huoni tofauti mwilini mwangu?” nilimuuliza.

“Hapana! Hebu niambie, kuna nini?”

Nikamwadithia kila kitu kilichotokea katika ndoto ile, yeye mwenye alishangaa kwamba ilikuwaje niote nafanya mapenzi halafu nimeamka na kujikuta kweli nikiwa nimefanya mapenzi.

“Labda majinamizi! Hebu ngoja nikupeleke nyumbani kwako,” aliniambia.

“Hapana! Kwanza subiri tuongee…”
“Hakuna tatizo! Ila unatakiwa kula kwanza.”

Nilikula, kilikuwa chakula kitamu sana ambacho sikuwahi kula hapo kabla. Kila mara nilikuwa nikimwangalia tu usoni mwake, alionekana kuwa na furaha kubwa isiyo kifani.

Baada ya kumaliza kula, nilijisikia kushiba na kuchka mwili hivyo kulala huku tayari ikiwa imetimia saa nane na nusu. Sikujua kitu gani kiliendelea lakini kilichonishangaza baada ya kuhstuka nikajikuta nikiwa nyumbani kwangu, tena kitandani kwangu.

Kwanza nikashangaa, sikujua nilifikaje nyumbani kwangu. Pembeni yangu alikuwepo Majeed, nilikuwa na swali hilohilo, ilikuwaje niwepo nyumbani na wakati hata Majeed hakuwa akipafahamu.

“Nani kanileta?” nilimuuliza Majeed huku nikimwangalia kwa mshangao.

“Mimi!”

“Umepajua vipi nyumbani kwangu?’ nilimuuliza huku nikimdadisi.

“Ulinielekeza!”

“Nilikuelekeza! Lini?”

“Hukumbuki?”
“Hapana! Sijawahi kukuelekeza nyumbani kwangu!” nilimwambia huku nikiwa na uhakika kwamba kweli sikuwahi kumuelekeza kabisa nyumbani kwangu.

Hakusema kitu zaidi ya kutabasamu tu, sikuacha kujiuliza juu ya kilichokuwa kimetokea, wakati mwingine nilihisi kwamba kila kitu kilichokuwa kikiendelea nilikuwa katika ndoto moja ndefu lakini haikuwa hivyo.

Siku hiyo nilitulia nyumbani, Majeed hakutaka kulala bali akaondoka zake. Nilikuwa kwenye mawazo tele, siku hiyo haikuwa nzuri kwangu kwani kulikuwa na vitu vingi nilivyokuwa nikijiuliza kuhusu huyu Majeed.

Siku iliyofuata nikaanza kupanga mipango yangu ya maisha kama kawaida, nilifikiria zaidi kuchuma fedha hata kabla sijafa na kuzikwa. Ulipokuwa ukifika wakati wa usiku, ilikuwa ni lazima nielekee katika chumba nilichokuwa nikihifadhi vitu vyangu vya kishirikina na kisha kufanya mambo ambayo yananipasa kufanya siku hiyo.

Ndani ya chumba hicho hakuruhusiwa kuingia mtu yeyote yule, kilikuwa ni chumba cha siri ambapo ndani yake kulikuwa na vitu ambavyo watu wengine wasingeweza kujua kazi yake.

“Unataka nini nikufanyie siku ya leo?’ nilisikia sauti kichwani mwangu, haikuwa sauti ya yule aliyekuwa akizungumza kipole, ilikuwa ni sauti ya yule aliyekuwa akizungumza kiukali.

“Ninataka kufahamu kitu kimoja.”
“Kipi?”
“Kuhusu huyu Majeed.”
“Unataka kujua nini kuhusu yeye?”
“Ni binadamu wa kawaida au si binadamu!” nilijibu.

“Hahaha!” Nilisikia kicheko kutoka kwake, sikujua kicheko hicho kilimaanisha nini. Nikashangaa.

****

“Kuna mambo mengine kuyajua ni vigumu sana, hasa kwenu wanadamu,” niliisikia sauti hiyo.

“Kivipi?”
“Kwa sababu ni mambo hayo yapo juu yenu.”
“Ila sijajibiwa kama Majeed ni binadamu au siyo!”

“Ni binadamu!” alinijibu.

“Binadamu?”
“Ndiyo! Kama wewe!” aliniambia.

“Inawezekana vipi akawa binadamu?”
“Na inawezekana vipi akawa si binadamu?” aliniuliza.

Kwa kweli nilichanganyikiwa, sikujua ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea. Niliambiwa kwamba alikuwa binadamu lakini matendo yake yalinitia hofu kubwa moyoni mwangu.

Nilibaki ndani ya chumba kile huku nikiambiwa mambo mengi sana, huyo aliyekuwa akiniambia maneno hayo yote akaniambia suala ambalo liliniweka kwenye wakati mgumu sana, akaniambia kwamba kama ninataka kwenda kuzimu, niliruhusiwa ila kulikuwa na vitu nilitakiwa kufanya.

“Niende kuzimu?” niliuliza.

“Ndiyo! Huku ni kwetu, utajiri uliokuwa nao umetoka huku, sisi ndiye tunatawala dunia kwa sasa na hakuna zaidi yetu,” niliisikia sauti hiyo.

Kwa kweli niliogopa sana, sikuamini kile nilichoambiwa. Nilitaka utajiri tu, kumwabudu shetani halikuwa tatizo lakini kitendo cha kuambiwa kwamba kama ningetaka kwenda kuzimu niliruhusiwa, sikutaka kukubaliana nacho kabisa, sikuwahi kufikiria kwenda huko katika maisha yangu.

“Unaogopa?” niliulizwa.

“Hapana! Ila siwezi kwenda huko!” nilijibu kwa kujiamini.

Huo ndiyo ukweli, sikutaka kwenda huko, ukiniuliza kwa sababu gani, sikuwa na jibu ila ukweli ulibaki huohuo kwamba sikutaka kwenda huko. Siku hiyo nilizungumza naye mambo mengi sana na kisha kutoka chumbani mule na kuufunga mlango.

Niliendelea na maisha yangu kama kawaida, utajiri ulizidi kuongezeka kama kawaida. Nakumbuka kuna siku niliambiwa kwamba nilitakiwa kutoa kafara, ilikuwa siku ya sikukuu ya kusherehekea miaka mita nane ya dini hiyo ambayo iliiteka dunia.

Nikaambiwa kwamba nilitakiwa kutoa kafara ya watoto wanne, wote hao walitakiwa kufa ndani ya nyumba yangu. Kwa kweli nilichanganyikiwa, sikujua ni kitu gani litakiwa kufanya.

Niliambiwa hivyo kwa kuwa tayari nilionekana kuwa na ujanja mkubwa wa kuwapata watoto wadogo na ndiyo maana waliamua kunitumia ila idadi waliyonipa ilikuwa kubwa mno.

Unapoambiwa kitu katika dini hiyo, hutakiwi kusema kwamba huwezi, unatakiwa kukubaliana nao na hata ikitokea umeshindwa, watakuelewa kuliko kusema huwezi.

“Nitawapa vipi hao watoto?” nilijiuliza swali nililokosa jibu kabisa.

Ni kweli mbele yangu kulikuwa na kazi kubwa lakini nilitakiwa kupambana nayo, watoto hao walitakiwa haraka iwezekanavyo hivyo nilichokifanya ni kuwasiliana na baadhi ya vyuo vya madrasa kwa lengo la kuja nyumbani kwangu na kupiga madufu kwa kisingizio cha kumuombea dua baba yangu ambaye alikwishakufa kitambo ili huko alipo Mungu amtangulie.

Kumbuka nilikuwa tajiri, maustadhi wa vyuo mbalimbali walivyosikia kuhusu kuhitaji vyuo vya kuja nyumbani kwangu kupiga kwa ajili ya dua, wakaomba nafasi na hatimaye kuwa na vyuo kumi na sita katika orodha yangu.

Kwa kweli nilifurahi sana na kuona kwamba kazi isingekuwa ngumu hata mara moja, nilifurahi sana kwani kazi ile ambayo kwa wengine ilionekana kuwa ngumu, kwangu ilikuwa nyepesi sana.

Siku zikasogea, nikaanza kuwaalika watu wengine wengi waweze kuhudhuria katika dua hiyo maalumu iliyotakiwa kufanyika nyumbani kwangu. Marafiki zangu wakaahidi kuja hivyo kilichokuwa kikisubiriwa kilikuwa ni siku husika tu, niue watoto wanne kisha kuwatoa kafara.

“Una uhakika utafanikiwa?” aliniuliza rafiki yangu mmoja ambaye naye alikuwa mwanachama katika dini hiyo.

“Ndiyo! Si kazi kubwa.”
“Utafanikiwa vipi?”
“Utaona tu.”
Hivyo ndivyo nilivyomwambia, sikutaka kumwambia mtu yeyote namna ambavyo ningefanikiwa kufanya kile nilichotaka kufanya. Siku zikasogea na hatimaye siku ya tukio hilo kufika.

Nakumbuka wakati wanachuo walipokuwa wakifika nyumbani hapo, naye Majeed alifika na moja kwa moja kuja chumbani kwangu. Siku hiyo alionekana kuwa mwenye furaha sana kiasi kwamba nikashangaa na kuhisi labda kulikuwa na kitu kilichokuwa kimemtokea.

“Kuna nini?” nilimuuliza.

“Hakuna kitu!”
“Mbona una furaha hivyo?”
“Hata mimi mwenyewe nashangaa mpenzi,” alinijibu. Sikutaka kubaki mahali hapo, nikamwambia kwamba ninakwenda nje mara moja hivyo anisubiri, ukweli ni kwamba sikwenda nje bali nilikwenda katika chumba kile kufanya maandalizi juu ya kile nilichotaka kukifanya wakati huo. Huku kila kitu kikiendelea, vyuo kadhaa vilikuwa vikifika nyumbani hapo hivyo kuwa na uhakika kwamba kila kitu kingekwenda sawa kama nilivyopanga.

****

Nilianza kufanya maandalizi ndani ya chumba kile, ilitakiwa watoto wanne wafe siku hiyo, haikujalisha kama ni ndani ya nyumba hiyo au nje lakini ilikuwa ni lazima wafe kama ilivyotakiwa.

Nilibaki chumbani humo kwa dakika kadhaa nikiandaa mazingira vizuri kwa ajili ya kufanya unyama huo wa ajabu. Nilichukua kioo na kukisimamisha kisha kuchukua unga fulani niliopewa na kuuweka kwenye ncha ya kisu.

Nilipofanya hivyo, nikasimama na kuanza kuzungumza maneno ambayo niliambiwa kama tu ningetaka taswira ya mtu niliyetaka kumuua ionekane ndani ya kioo hicho. Nilizungumza kwa dakika kadhaa na ndipo nikaanza kuwaona watu wakiingia ndani ya nyumba yangu.

Moyo wangu ulikuwa na faraja tele, niliamini kwamba ningefanikiwa kwa asilimia mia moja hivyo sikutakiwa kuwa na hofu hata mara moja. Chumbani humo nilikaa kwa dakika kadhaa na ndipo nikatoka huku kila kitu kikiwa tayari kabisa.

“Umetoka wapi?’ aliniuliza Majeed.

“Jamani mpenzi! Kwani nilikwambia nakwenda wapi?” nami nilimuuliza swali.

“Aya, achana na hayo! Ratiba ipo vipi?” aliniuliza tena.

“Ipo kawaida, vyuo vipige na baada ya hapo, chakula na watu waende kwao,” nilimjibu huku nikjifanya kuwa bize kufanya vitu vingine hali iliyoonyesha kwamba sikutaka kusikia kitu kingine kutoka kwake.

Hakuwa muongeaji sana hivyo akaniacha niendelee kufanya mambo yangu na nilipomaliza tu, tukatoka kwenda nje ambapo kulikuwa na idadi kubwa ya watu. Waliponiona, wakaanza kunishangilia, nikachukua kipaza sauti na kuanza kuzungumza nao.

“Nashukuru kwa kuitikia mualiko wangu, hakika mmenifariji sana, nimejisikia kuthaminika zaidi ya mnavyofikiria,” niliwaambia huku nikiwaangalia nyusoni mwao.

Hakukuwa na muda wa kupoteza, nikamwambia mc aanze shughuli hivyo ikaanza kupiga madrasa moja kutoka Temeke, kila mmoja alionekana kufurahi sana kwani kilikuwa ni kitu wasichokitarajia kukutana na mimi ambaye kwa kipindi hicho nilikuwa na fedha sana.

“Huu ni wakati wangu,” nilijisemea.

Sikutaka kusubiri, nilichokifanya ni kuanza kutembea huku na kule huku nikitaka kumtoka Majeed ambaye siku hiyo sijui kwa nini kwani alitokea kuniganda sana.

Nilifanikiwa kumtoka na hivyo kuelekea katika chumba kile ambapo baada ya kufika, nikachukua kisu kilichokuwa sakafuni na kisha kusimama mbele ya kioo kile, nikaanza kuongea maneno yaleyale ambayo leo hii ukiniuliza yalikuwa maneno yapi, siwezi kukumbuka.

“Ninataka kuua watoto wanne, naomba unisaidie bwana wangu,” nilijisemea huku nikiwa nimeshika kisu hicho mkononi mwangu.

Hapohapo picha za watoto wale wakiwa kule uwanjani ikatokea, ilikuwa ni idadi ya watoto wengi hivyo kuchagua watoto wanne ambapo hapohapo nikachukua kisu na kuchoma taswira za watoto wanne ambao nilitaka wafe kama nilivyotaka.

“Tayari, nimekamilisha kazi yangu,” nilijisemea na kisha kutoka.

Nilichokuwa nikijua ni kwamba watoto hao wangekufa hapohapo nyumbani kwangu kumbe mambo hayakuwa hivyo. Nilirudi mpaka kule uwanjani, hakukuwa na mtoto yeyote aliyekufa hivyo kushangaa sana.

“Imekuwaje? Mbona hakuna aliyekufa?” niliuliza huku shughuli ikiendelea.

Shughuli iliendelea kwa muda wa saa mbili, ilipomalizika, watu wa chakula walikuwa wamekwishafika na chakula kingi na cha kutosha na kuanza kula. Muda wote nilikuwa nikiangalia huku na kule, nilikuwa nataka nione kama kile nilichokifanya chumbani kilifanikiwa au la.

“Vipi mpenzi! Mbona unaonekana hivyo?” aliniuliza Majeed huku akiniangalia usoni.

“Nipo vipi?”
“Unaonekana kuwa na mawazo mengi, tatizo nini?” alinitupia swali.

“Hakuna kitu! Labda nimemkumbuka baba,” nilimjibu, akaniangalia, halafu akacheka.

Watoto wote wakaaga na kuondoka huku akiwa hajafa hata mtoto mmoja. Nikaelekea chumbani, bado nilikuwa na mawazo kwamba kwa nini kile nilichotaka kitokee hakikutokea na wakati nilifanya kila kitu kwa usahihi?

Wakati nikiwa chumbani humo huku nikiwa na maswali mengi kichwani mwangu, nikasikia simu yangu ikianza kuita. Nikaichukua na kuanza kuangalia kioo, alikuwa mmoja wa maustadhi wa vyuo vile vilivyokuja nyumbani kwangu, nikaipokea na kuipeleka sikioni.

“Kuna nini tena?” niliuliza mara baada ya kusikia watu wakilia.

“Kuna ajali imetokea!” alinijibu.

“Kuna ajali imetokea? Wapi?” niliuliza kwa kuhamaki.

“Hapana Magomeni! Tumejeruhiwa vibaya, watoto wanne wamekufa hapahapa,” niliisikia sauti ya ustadhi huyo, bado nusu nishangilie kwani mshtuko wa furaha ulionipata, haukuweza kufanikiwa.

“Mungu wangu! Mpo wapi sasa hivi?” niliuliza.

“Muhimbili!” alijibu, nilichokifanya ni kutoka ndani na kuanza kuelekea huko Muhimbili. Nilitaka kwenda kuwafariji japokuwa mimi ndiye niliyesababisha ajali hiyo!

****

Nilikuwa ndani ya gari nikiendesha gari kwa kasi ya kawaida, kichwa changu kilikuwa kikifikiria kile kilichokuwa kimetokea, sikuamini kama kweli mambo yalikwenda kama yalivyotakiwa kwenda kwani kwa akili ya kibinadamu nilifikiri kwamba watoto wale wangekufa nyumbani kwangu.

Kutoka hapo nyumbani kwangu mpaka katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili nilitumia muda wa dakika ishirini, nikafika na moja kwa moja kupaki gari langu na kuelekea ndani ya wodi moja hapo hospitali.

“Kuna nini ustadhi?” nilimuuliza ustadhi ambaye nilimkuta hospitalini hapo na baadhi ya wanafunzi wa madrasa.

“Tulipata ajali mbaya ya gari,” alinijibu, sauti yake tu niligundua kwamba hata yeye pia alikuwa kwenye maumivu makali mwilini mwake.

“Poleni sana, ilikuwaje?’ nilimuuliza.

“Tulikuwa tukipita katika Barabara ya huku Tandale Uzuri, tulipofika Tandale kwa Tumbo, mbele yetu hakukuwa na gari, na tuliamini kwamba hakuna gari, cha ajabu, ghafla tukaliona gari likishuka kilima kutoka Popobawa na kuja kutugonga kwa mbele, tumepoteza watoto wanne,” alisema ustadhi huyo na kuanza kulia.

Moyo wangu ukafarijika, hicho ndicho nilichotaka kusikia kwamba watoto walikufa kama ilivyotakiwa. Kwa kuwa sikutaka kugundulika kama mimi ndiye niliyehusika katika ajali ile, muda wote nilionekana kuwa kwenye mawazo tele, nilijifanya kuumia moyo lakini ukweli ni kwamba nyuma ya pazia, nilikuwa na furaha mno.

Baada ya dakika kadhaa ndugu wa marehemu wakafika hospitalini hapo. Walikuwa wakilia, waliguswa na msiba wa ndugu zao, nilivyokuwa nikiwaangalia jinsi walivyolia, moyo wangu uliniuma na huruma ikauingia moyo wangu.

Sikuweza kubadilisha kitu chochote kile, halii ilitakiwa kubaki vilevile kwamba watoto wale walikuwa wamekufa na hivyo walitakiwa wandelee na maisha yao likiwemo suala la mazishi.

“Poleni sana,” niliwafariji wafiwa.

Kesho yake tu mazishi ya watoto wte yakafanyika. Msibani kulikuwa na watu wengi sana, misiba minne kwa pamoja iliwavuta watu wengi, wengi wakalaani ajali ambazo kwa kipindi hicho zilishika kasi sana.

Baada ya kumaliza kila kitu nikarudi nyumbani kwangu. Siku hiyo nilimkuta Majeed akiwa sebuleni, sikujua alikuja muda gani ila kwa jinsi nilivyomwangalia, alionekana kuwa na furaha sana.

Nilitaka kujua chanzo cha furaha yake, hivyo nikamuuliza lakini hakutaka kuniambia, alichokisema ni kwamba alishtuka akiwa na furaha, ila chanzo cha furaha yake, hakuwa akijua.

“Nahisi kuna kitu,” nilimwambia.

“Hakuna kitu mpenzi! Kama kuna kitu, kwa nini nisikwambie!”

“Mmh! Aya bwana kama unanificha,” nilimwambia huku nikiachia tabasamu pana.

Sikutaka kujali sana kwani nilijua kwamba Majeed alikuwa muongeaji sana, nilichokifanya ni kuondoka na kuelekea bafuni kuoga, huko, nilijiona kuwa shujaa mkubwa, kitendo cha kuwaua watoto wanne kwa ajili ya kuwatoa kafara ilinifurahisha sana.

Nilipomaliza kuoga, nikarudi chumbani na kutulia kitandani. Bado nilionekana kuwa mwenye furaha kubwa kupita kawaida. Wakati nimetulia hapo kitandani huku nikipiga stori na Majeed, nikahisi ghafla mwili ukichoka sana, wala haukupita muda mrefu, usingizi mzito ukanichukua.

Kilichofuata kilikuwa ni kuota ndoto. Niliota nikiwa nimekwenda hospitalini huku nikiwa na Majeed, alionekana kuwa mwenye furaha tele kuliko hata mimi. Sikujua sababu ya mimi kuwa hapo hospitali pamoja naye.

Tulikaa kwenye benchi na kumsubiria daktari ambaye baada ya dakika chache tu, akatokea na kutuambia tuingie ndani, mpaka tunaingia humo, sikuwa nikijua sababu iliyotufanya tuwe hapo.

“Unasema unahisi mke wako ana mimba?” aliuliza daktari huku akimwangalia Majeed.

“Ndiyo!” alijibu.
Wakati ametoa jibu hilo mimi mwenyewe nilikuwa nikishangaa, kwanza sikujua kabla sababu ya kuwa hapo, sasa ilikuwaje ahisi mimi nina mimba na wakati hata hisia hizo sikuwahi kuzisikia mwilini mwangu.

“Nina mimba?” niliuliza huku nikionyesha mshttuko.

“Ndiyo mpenzi! Una kila dalili!”

“Hapana! Sina mimba!”

“Subiri kwanza daktari akupime!”

“Sawa! Ila sina mimba!” nilisema.

Sikujua ni muda gani alichukua mkojo wangu, nilichoshtukia ni kwamba alikuwa nao katika kichupa kidogo, alipima na baadaye kuja na majibu kwamba kweli nilikuwa na mimba.

Nilishangaa sana, ilikuwaje niwe na mimba? Labda kwa sababu nilifanya mapenzi na Majeed, hiyo mimba ilikuwa ni ya nani? Ya kwake au? Yote hayo nilijiuliza lakini sikupata jibu.

Majeed akatoa tabasamu pana na kisha kunikumbatia, maneno niliyoweza kuyasikia ni “Asante mke wangu kwa kubeba mtoto wangu.”

Nikashtuka kutoka usingizini. Majeed alikuwa pembeni yangu huku akitabasamu. Nikashangaa.

****

“Kuna nini tena?” aliniuliza Majeed huku akiniangalia usoni.

“Nimeota.”
“Ndoto gani? Umekufa?” aliniuliza.

“Hapana! Eti nina mimba!”

“Hahaha!”

“Unacheka nini sasa?”
“Nimefurahi tu! Kwani kuwa na mimba ni tatizo mpaka uamke huku ukiweweseka?” aliniuliza huku akiniangalia.

Sikuwa na la kumjibu ila ndoto hiyo ikanifanya kuwa na wasiwasi sana, sikuwahi kufanya mapenzi na Majeed zaidi ya ndotoni tu, niliichukulia kuwa ndoto ya kawaida kama ndoto nyingine.

Nililiangalia tumbo langu, lilikuwa kawaida tu lakini sasa kitu kilichonishangaza, baada ya wiki kupita, nikaanza kuhisi hamu ya kula vitu vichachu huku nikianza kutapika.

Nilishangaa mno, nilizipata dalili hizi za kuwa na mimba, zilinichanganya sana kwani tangu nifanye mapenzi na Mudi kipindi cha nyuma ambapo ilipita miezi mingi sana, sikuwahi kufanya mapenzi na hata Majeed sikuwahi kufanya naye kwa kuwa alikuwa akikataa, sasa iweje niwe na mimba.

Nilichanganyikiwa hivyo nilichofanya ni kwenda hospitali, nilitaka kwenda kupima nione kama nilikuwa na mimba au la kwani dalili zilizokuwa zikionekana katika mwili wangu, zilionyesha kabisa kwamba nilikuwa na mimba.

“Una uhakika kwamba una mimba?” aliniuliza daktari.

“Ndiyo! Nina kila dalili za mwanamke mjauzito dokta,” nilimwambia.

“Sawa! Subiri nichukue vipimo,” aliniambia na kisha kuniambia nikamletee mkojo wangu, nikafanya hivyo.

Nilikaa nikisubiri majibu, muda mwingine Majeed alikuwa akinipigia simu lakini sikutaka kupokea, sikutaka kumwambia kuhusu zile dalili nilizokuwa nikiziona kwani zingemfanya kuwa na wasiwasi na mimi.

Baada ya dakika kadhaa, daktari akaniita katika ofisi yake na kuniambia kwamba sikuwa na mimba kama nilivyokuwa nikihisi. Nilichanganyikiwa sana, sikuridhika, nilichokifanya ni kupima magonjwa mengine, kote nilionekana kuwa salama.

“Sasa tatizo nini?” nilimuuliza daktari.

“Hata mimi nakushangaa unaposema unaona dalili za mimba na wakati huna mimba. Hebu nikuulize swali, mara yao ya mwisho kufanya mapenzi ilikuwa lini?” aliniuliza.

“Miezi kumi iliyopita!”
“Miezi kumi iliyopita?”
“Ndiyo!”
“Sasa inawezekanaje hili? Ushawahi kuoga kwenye swimming pool?”

“Hapana!”

“Mmh!”

“Ndiyo hivyo! Yaani hapa nimechanganyikiwa.”

Sikutaka kuendelea kubaki hapo hospitali, nilichokifanya ni kuondoka na kurudi nyumbani, njiani nilikuwa na mawazo mengi, kichwa changu kiliniuma sana kwani kile kilichokuwa kikiendelea hakika kiliniweka katika wakati mgumu sana.

Nilipofika nyumbani, nikajifungia chumbani na Majeed kuja nyumbani, alipofika, yeye mwenyewe alihisi kwamba kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea, akaniuliza sababu ya kuwa hivyo lakini sikumwambia ukweli, nilichomwambia ni kwamba nilikuwa nikijisikia vibaya tu.

“Kuna mambo mengi unanificha siku hizi, kwa nini?’ aliniuliza Majeed huku akiniangalia usoni.

“Hakuna lolote mpenzi!”

“Hapana! Unakosea, kama mimi unanificha, nani utamwambia?” aliniuliza.

“Hakuna kitu mpenzi!”
“Una uhakika?”
“Ndiyo!”
“Unaumwa?”
“Hapana!”
“Ulikwenda hospitalini kufanya nini?” aliniuliza.

Nilishtuka sana, sikuamini kama alikuwa akijua kile kilichokuwa kimetokea kwamba nilikwenda hospitalini. Sikumwambia lakini kitu cha ajabu, alijua hilo. Sikumjibu, nilikuwa kimya huku nikimwangalia tu kwani hata mdomo kufunguka ulikuwa mzito.

“Mimi kwenda hospitalini!”
“Pia unataka kukataa! Au mpaka nikwambie ulikwenda kufanya nini, ulikutana na daktari gani, alikupima nini na majibu yalikuwaje?” aliniuliza.

Hapo ndipo akanichanganya zaidi. Nilichanganyikiwa mno, ilikuwaje huyu Majeed ajue kila kitu kilichokuwa kimetokea. Nilishindwa kumficha kwani kweli alionekana kufahamu kila kitu kilichotokea, huo ukawa muda wangu wa kumwambia ukweli.

“Ndiyo nilikwenda, ninahisi nina mimba, nimekwenda hospitali, cha kushangaza, sikuonekana kuwa na mimba,” nilimwambia, sikuwa na jinsi.

“Hizo dalili zimeanza lini?” aliniuliza.

“Siku hizi mbili, tena zimeanza baada ya kuota kuwa na mimba yako,” nilimwambia Majeed.

“Acha utani, yaani uote una mimba, halafu dalili zionekane kweli!”

“Ndiyo hivyo!”

Tulibaki tukizungumza kama wapenzi, siku ziliendelea kukatika, ndoto za kuwa na mimba ziliendelea kunitesa sana. Kila nilipoota, niliota nikiwa na Majeed na kisha kulibusu tumbo langu ambalo lilianza kuwa kubwa.

Nilishangaa sana, nilipokuwa nikiamka, sikuwa na mimba yoyote ile. Miezi ikakatika na hatimaye mwezi wa nane kuingia, tumbo likawa kubwa ndotoni ila kilichonipa maswali zaidi, mbona kwenye ulimwengu wa kawaida sikuwa na mimba. Kwa kweli nilichanganyikiwa.

****

Baada ya siku kadhaa kupita, hatimaye mimi na wenzangu tuliweza kurudi tena katika kanisa letu la kishetani huku tukiwa na mafanikio makubwa. Ndugu zangu, ninazungumza haya ambayo niliyaona kwa kipindi kirefu nikiwa huko.

Dunia hii tunayoishi kuna mambo mengi sana yanatokea, kuna mengi yanaendelea na yanaendeshwa katika ulimwengu wa kishetani. Kuna manukato huwa tunajipulizia, tena yale ambayo watu wanasema kwamba ni mazuri, yananukia vizuri sana lakini ukweli ni kwamba yanatengenezwa kuzimu na kabla ya kuuzwa, huwa yanaletwa katika kanisa hilo na kisha kuyawekea mikono.

Tembelea madukani, utakutana na manukato ambayo muuzaji anakwambia kwamba ukijipulizia kwa mwanaume, kila mwanamke ukipishana naye anakupenda, au kama ni ya mwanamke, ukijipulizia, wanaume wanakupenda.

Sizungumzi haya kwa nia mbaya, ninazungumza kwa kuwa ninataka ujue kile kinachoendelea katika ulimwengu mwingine. Kazi inayofanyika ni kubwa sana, kuna mitindo ya nguo mingi inaingia duniani ambapo bila kujua, huwa tunaivamia na kuvaa au hata kusuka kichwani.

Ndugu zangu, nisingependa kuizungumzia mitindo yote ila jua kwamba shetani yupo kazini, mitindo mingi ya jinsi, kubana, kutobokatoboka, hutoka huko, na huletwa duniani kwa kuwa bado shetani ana kazi kubwa ya kufanya katika dunia hii.

Labda mwanaume unamuona mwanamke kuwa wa kawaida, lakini anapovaa suruali ya jinsi, iliyombana, unajikuta ukimpenda tu, unajua kwa nini? Zamani nilihisi ni kawaida kumbe kuna vitu vinawekwa katika nguo hizo ambavyo vinamfanya mwanaume avutike hata kama hampendi mwanamke, nyuzi nyembamba zinapitishwa katika nguo hizo, na mwanaume unapomwangalia mwanamke lazima umtamani.

Ukiachana na hivyo, pia kuna magari! Wanawake wengi wanapenda wanaume wenye magari, kwenye magari hayohayo, asilimia kubwa yanapitia katika mikono ya kuzimu na kuwekwa mambo ya ajabu. Utakuta mwanamke kwao wana magari kama kumi, tena ya gharama ila mwanaume akija na gari ya gharama, anamchukua mwanamke, kisa gari, si kwamba gari tu, ndani ya gari kuna vitu ambavyo vimewekwa, mwanamke hawezi kuvijua au kuviona, huwa anajikuta akipenda magari.

Nilibaini mambo mengi katika ulimwengu huo, nilitoka huko kitambo na ndiyo maana nimeamua nikwambie mambo mengi yanayoendelea huko katika ulimwengu mwingine.

Kumbuka niliwatoa watoto wanne kafara, wale watoto waliokuja kupiga madufu nyumbani kwangu, hapo katika kanisa la shetani, wale watoto wakawekwa mbele na kisha kuanza kuchinjwa mmoja baada ya mwingine na damu zao kuwekwa kwenye vikombe na kunywa.

Maisha haya yalinitesa kipindi cha nyuma lakini nikawa nimekwishazoea, tamaa yangu ya kutaka utajiri ikanifanya kuingia katika ulimwengu huo wa ajabu.

Maisha yangu yaliendelea, katika ulimwengu wa kawaida, sikuwa na mimba lakini kila nilipokuwa nikilala, niliota ndoto nikiwa na mimba, tena ikiwa changa mpaka ilipokuwa kubwa, mimba ya mwanaume, mpenzi wangu Majeed ambaye sikuwahi kufanya naye mapenzi katika ulimwengu wa kawaida, alikataa ila nilipokuwa nikilala, niliota nafanya naye mapenzi na mwisho wa siku kupata mimba hukohuko ndotoni.

“Huyu Majeed ni nani? Ni jini au? Na kama ni mtu wa kawaida, mbona naota sana nikiwa naye na amenipa mimba? Ila kama nina mimba tena tumbo likiwa kubwa, mbona katika maisha halisi sina mimba? Nini kinaendelea?” nilijiuliza sana lakini sikupata jibu.

Hakukuwa na kitu kilichokuwa kikinitesa katika wakati huo kama suala la mimba, ndoto nilizokuwa nikiziota zilikuwa ni juu ya ile mimba niliyokuwa nayo huko, kila nilipomwambia Majeed, aliniambia kwamba nisiwe na hofu yoyote ile kwani hiyo ilikuwa ndoto tu na haikuwa na maana yoyote ile.

“Ila Majeed mpenzi!” nilimwambia.

“Mpenzi, wala usiogope, ni suala la ndoto tu,” aliniambia huku akiachia tabasamu lake, alijua fika kwamba hiyo ndiyo ilikuwa silaha yake kuu, na kweli iliniumiza sana kwani hata nilipokuwa na wasiwasi, wasiwasi wote juu yake ukaondoka.

Nakumbuka siku moja nilikuwa nimelala usiku, nilianza kuota ndoto kama kawaida. Nilianza kushikwa na uchungu wa kuzaa, sikuwa na msaada wowote ule kwani pale nyumbani nilikuwa peke yangu.

Nilibaki nikiugulia kwa maumivu makali, mfanyakazi wangu wa ndani hakuwepo pia, alikuwa amekwenda sokoni. Wakati nikiwa kwenye uchungu huo wa kuzaa, kwa bahati Majeed akatokea na hivyo kunisaidia kwenda hospitali.

“Vumilia mpenzi! Vumilia utajifungua salama,” aliniambia huku akiendesha gari.

Tulifika katika Hospitali ya Muhimbili salama kabisa, akanifungulia mlango na kuniteremsha kisha kuwaita manesi ambao walifika na kisha kunipandisha kwenye machela na kunipeleka leba.

Majeed alinisubiri nje mpaka pale nilipojifungua, nikapelekwa katika chumba cha mapumziko ambapo baadaye akaja na kunijulia hali. Nilijifungua mtoto mzuri wa kiume aliyempa jina la Zakeed likiwa na muunganiko wa majina yetu yote mawili.

“Unajisikiaje?” aliniuliza huku akiniangalia.

Nilipotaka kujibu swali lake, ghafla nikashtuka kutoka usingizini, nikaanza kuangalia huku na kule, ilikuwa ni usiku wa saa nane, nilijiuliza ilikuwaje? Kitu cha kwanza nilichokifanya ni kuangalia tumbo langu, lilikuwa kawaida, ila cha ajabu nilipoangalia maziwa yangu, yalikuwa makubwa kama mwanamke aliyezaa, na nilipoyabinya, cha kushangaza yakatoa maziwa, hakika nilishtuka!

****

Kilikuwa kitu kilichonishangaza sana juu ya maziwa yangu, nilishindwa kuamini kwamba kile kilichokuwa kikiendelea katika ndoto, kweli kiliendelea mpaka katika maisha yangu halisi.

Nilichanganyikiwa na Majeed alipokuja asubuhi, nilimueleza ukweli kile kilichokuwa kimetokea, yeye mwenyewe alichanganyikiwa, hakumini kama kitu hicho kingeweza kutokea.

“Haiwezekani!” aliniambia huku akiniangalia.

“Kweli! Angalia,” nilimwambia na kumuonyeshea, kweli maziwa yalikuwa yakitoka.

Alichonifanya ni kunichukua na kunipeleka hospitalini. Tulipofika, tukaenda na kumuona daktari, yeye mwenyewe alishangaa, hakuamini kile alichokiona, inakuwaje msichana hujazaa halafu maziwa yakawa yanatoka kwa wingi kiasi hicho?

“Ulikuwa mgonjwa?” aliniuliza.

“Hapana!”

“Ushawahi kuzaa huko nyuma?”
“Hapana!”
“Kutoa mimba je?”
“Hapana!”

Daktari alibaki akiwa amepigwa bumbuwazi, akanichukua na kunipima vipimo vingine na mwisho wa siku kuniambia kwamba hilo ni suala la afya kwani si mimii tu niliyekuwa nikipata tatizo hilo bali kulikuwa na wanawake wengi tu.

“Ni kweli?”
“Ndiyo! Wengi hupata tatizo hilo! Litakwisha tu,” aliniambia huku akiwa amenikazia macho.

Tukaondoka na kurudi nyumbani. Nikiwa njiani, niliamua kumuuliza Majeed juu ya hali iliyokuwa ikiendelea kwamba kwa nini hakutaka kufanya mapenzi na mimi na wakati tulikuwa wapenzi wa muda mrefu.

Hakulipenda swali hilo lakini akajifanya kunionyeshea tabasamu pana. Kichwa changu kilichanganyikiwa, moyo wangu uligawanyika, upande mmoja wa moyo uliniambia kwamba Majeed alikuwa jini lakini upande mwingine ukaniambia kwamba alikuwa binadamu wa kawaida.

“Wewe ni nani?’ nilimuuliza huku nikiwa nimemwambia asimamishe gari pembeni.

“Kivipi?”
“Wewe ni binadamu au?” nilimuuliza.

“Kwa nini umeuliza hivyo?”
“Kwa sababu nataka kujua. Niambie ukweli, hata kama ni jini, niambie ukweli tu. Nitakuwa na amani,” nilimwambia.

Kabla ya kunijibu, akatoa kicheko na kuniangalia machoni, akanilegezea macho kama msichana na kuniambia nisiwe na hofu kwani kila kitu ningejua tu bila tatizo lolote lile.

Sikutaka kukubali, nilivumilia sana, siku hiyo ilikuwa ni siku ya kufahamu ukweli kwani hilo lilikuwa jambo lililouumiza mno moyo wangu. Nilijifanya kutokuelewa kitu chochote mpaka aniambie ukweli.

“Una uhakika hutoogopa?” aliniuliza.

“Siwezi!”
“Sawa. Mimi ni jini Mashbiri,” alinijibu huku akiniangalia.

“Wewe ni jini?” niliuliza huku nikiwa na mshtuko.

“Ndiyo! Mimi ni jini ninayependa binadamu, umekuwa msichana mzuri kwangu, niliweza kukufuatilia kwa kipindi kirefu sana, nilikuona mara ya kwanza ulipokwenda kaburini, ulikuwa msichana mzuri, uliyetafuta utajiri kwa nguvu zote, niliumia sana na ndiyo maana nikaamua kukufuata,” aliniambia.

“Kwa nini mimi?”
“Kwa sababu wewe ni mzuri!”
“Majeed! Na kuhusu suala la kufanya mapenzi?”
“Majini ya jamii yetu huwa hatufanyi mapenzi na binadamu, tunafanya nao kwenye ndoto kama ilivyokuwa kwako,” alinijibu.

“Kwa hiyo umefanya mapenzi na mimi ila ndotoni?”
“Ndiyo!”
“Na ukanipa mimba?”
“Ndiyo!”
“Na mtoto wangu yupo wapi?” nilimuuliza.

“Yupo kwa bibi yake.”
“Hapana! Ninataka kumuona mtoto wangu. Naye ni jini au binadamu?”

“Nusu jini, nusu binadamu,” alinijibu.

“Ninataka kumuona kwanza.”
“Sawa. Tutakwenda usiku!”
“Kwa nini usiku?”
“Na kwa nini sasa hivi?”
“Kwa sababu nataka nimuone!”
“Sawa. Ila ni usiku. Naomba uniamini, tutakwenda na wala usiniogope mpenzi,” aliniambia huku akinisogelea, akanibusu mdomoni, tulikuwa barabarani lakini baada ya kunipa busu hilo, ghafla nikajikuta nikiwa chumbani pamoja naye, cha kushangaza, eti tayari ilikuwa usiku.

“Upo tayari twende?” aliniuliza huku akiniangalia.

Hata kujibu ndiyo! Niliogopa.

Akaniambia kwamba nilitakiwa kujiandaa kwa ajili ya kwenda huko nyumbani kwao ila nisingeweza kwenda hivi bali kuna vitu ambavyo nilitakiwa kuvifanya.

Kwanza nilitakiwa kujipulizia manukato ya kuvutia lakini pia nilitakiwa kuwasha ubani chumbani kwangu kwani hayo ndiyo yalikuwa maandalizi makubwa ambayo yangewafanya wazazi wake wanipokee kwa furaha.

Hilo wala halikuwa tatizo hata kidogo, nikakubaliana naye na kufanya kama alivyotaka kufanya. Kwa kuniangalia, nilionekana kama kuwa na hamu ya kutaka kuona kile ambacho kingeendelea hivyo ilikuwa ni lazima nifanye hivyo.

Baada ya saa moja, kila kitu kilikuwa tayari, mavazi yangu yote yalinukia ubani, akanisogelea nilipokuwa na kunishika mkono. Ngozi yake ilikuwa laini sana kama ya mtoto kiasi kwamba nikashangaa.

“Upo tayari?” aliniuliza.

“Nipo tayari!”

Nilipojibu hivyo, akaniambia akaniambia nibane pumzi na kisha nifumbe macho, nikafanya hivyo na aliponiambia fumbua macho, nikashangaa kuona tukiwa baharini.

Akapiga hatua kadhaa mbele kuifuata bahari na kuniambia nimfuate, hakika niliogopa kwani ulikuwa ni usiku sana na mawimbi yalipiga mno. Nikapiga moyo konde na kumfuata kule alipokuwa akienda. Niliingia ndani ya maji kumfuata, tukaendelea mbele mpaka tulipoanza kuzama.

Nilipiga kelele na kumuomba anisaidie kwani nilipoanza kuzama, nilihisi kabisa nikivutwa, sikutaka kuelekea huko lakini ikashindikana. Wakati nikilia na kuomba msaada, ghafla nikajikuta nikiwa mahali fulani, hakukuwa sehemu ya kawaida hata kidogo, kulikuwa na hali fulani ya joto na hata hakukuwa na harufu nzuri hata kidogo.

Ulikuwa ulimwengu mwingine uliokuwa na majumba mengi mazuri, viumbe vya ajabu ambavyo vilinifanya kuogopa sana. Mbele yangu alisimama Majeed, nilipotaka kukimbia, akanishika mkono na kuniambia nisikimbie, ilinipasa nizoee mazingira niliyoyakuta mahali pale.

“Hapa ni wapi?’ nilimuuliza huku nikiogopa.

“Nyumbani kwetu!”

“Nyumbani kwenu? Wapi?” nilimuuliza, hakunijibu zaidi ya kutabasamu.

Tukaondoka mahali hapo. Sikujua kama hapo kulikuwa kuzimu, ulikuwa ulimwengu mwingine kabisa. Kama unavyoona kwamba huku kuna nyumba, hata huko zipo, kama shule, huko napo zipo kama huku.

Ulikuwa ulimwengu wenye kutisha na kusisimua, nilikuwa muoga sana kwani kwa vile nilivyokuwa nimekutana navyo humo, viliniogopesha sana. Tulitembea mpaka tulipofika katika nyumba moja kubwa, ilikuwa imenakshiwa dhabau kwa nje, tukaingia ndani.

“Karibu!” alisema msichana mmoja, alikuwa mzuri mno, Majeed akaniambia kwamba huyo alikuwa mfanyakazi wa ndani.

Nilishangaa sana kwamba kwa nini Majeed alinifuata mimi na wakati hapo kwao kulikuwa na mfanyakazi wa ndani aliyekuwa mrembo kama huyo. Sikuwa nimemuuliza swali hilo lakini nikashangaa akinijibu kwamba alipenda sana kuwa kwenye uhusiano na binadamu.

Nikakaribishwa ndani na kutulia kwenye masofa, palikuwa pazuri sana, nilijiachia mpaka baada ya dakika kadhaa watu wawili wazima wakafika na kutambulishwa kwamba walikuwa wazazi wake.

Nilisimama na kuwasalimia, walionekana kuwa na furaha sana. Hapo ndipo Majeed alipoanza kututambulisha. Nilifurahi kuwaona, walikuwa majini lakini muonekano wao ulikuwa ni wa kawaida sana.

Nilitulia hapo, baada ya sekunde chache nikasikia sauti ya mtoto akilia. Majeed akaniangalia, akaachia tabasamu na kuniambia kwamba aliyekuwa akilia alikuwa mtoto wangu wa kiume.

Nilishika na hamu ya kumuona, mara msichana mmoja mrembo akatokea mahali hapo, alikuwa mzuri wa sura kwa kweli, mkononi mwake alikuwa amebeba mtoto mdogo wa kiume na kumsalimia, nilipomwangalia mtoto huyo, nilifanana naye sana.

“Ni mtoto wangu?” niliuliza huku nikitabasamu.

“Ndiyo mpenzi wangu! Anafanana nawe sana,” aliniambia Majeed.

Nikamchukua na kumbeba. Mtoto yule akaachia tabasamu pana, hata kulia kule kukaacha kwani alitambua kwamba alikuwa katika mikono ya mama yake.

Ndugu yangu! Haya ninayokwambia, niliyaona katika safari yangu ndefu ya utajiri. Nilikaa katika ulimwengu huo kwa siku mbili ndipo nikarudi duniani kuendelea na maisha yangu.

Utajiri wangu ukaongezeka maradufu kwani wazazi wake Majeed waliamua kunitajirisha sana kwa kunipa dhahabu na mali nyingine nyingi. Nikazidi kupata sifa katika jamii inayonizunguka. Nikanunua mabasi makubwa ya mikoani, lengo la kununua mabasi hayo ni kutaka kutoa watu kafara kupitia ajali mbalimbali. Hilo ndilo lilikuwa lengo langu!

 

Je, nini kitaendelea?
Tukutane sehemu ya mwisho siku ya Jumatano.

Comments are closed.