The House of Favourite Newspapers

Niyonzima Anusurika Kupigwa Kisu India

Haruna Niyonzima.

KIUNGO wa Simba, Haruna Niyonzima amenusurika kufanyiwa oparesheni mguuni mwake baada ya vipimo vya uchunguzi wa jeraha lake kutoka na kuonyesha hakuna haja ya kupasuliwa.

 

Niyonzima, raia wa Rwanda, alisafiri Jumanne wiki hii kwenda India kufanyiwa matibabu ya jeraha lake alilolipata chini ya enka katika mguu wake wa kulia.

 

Jeraha hilo limemuweka Niyonzima nje ya uwanja kwa muda wa miezi miwili sasa tangu Desemba mwaka jana ikiwa ni miezi michache baada ya kujiunga na timu hiyo akitokea Yanga.

 

Akizungumza na Championi Jumamosi kutoka Hospitali ya Jeevika, India anapopatiwa matibabu, kiungo huyo alisema, kutokana na vipimo alivyofanyiwa hatofanyiwa operesheni tena, badala yake itatumika njia kumtibu.

 

“Namshukuru Mungu kwa kuepuka kufanyiwa oparesheni ndogo katika jeraha langu, madaktari wameniambia jeraha langu halihitaji oparesheni na badala yake watatumia njia nyingine ya matibabu ili nipone haraka.

 

“Nilipopimwa huko Dar es Salaam, ilionekana ni lazima nifanyiwe oparesheni, lakini huku India wamezuia kunifanyia oparesheni na badala yake watanipatia matibabu mengine mbadala na naamini nitakuwa fiti,” alisema Niyonzima.

 

Kiungo huyo alisema kwa matibabu ya siku tatu aliyofanya, ameona mabadiliko makubwa ya maendeleo ya jeraha lake huku akidai mapema atarejea uwanjani baada ya kunusurika oparesheni.

Stori: Wilbert Molandi, Dar es Salaam

Comments are closed.