NUH Afungukia Kubebwa na Shilole
MWANAMUZIKI Naftar Mlawa ‘Nuh Mziwanda’ ambaye aliwahi kufanya vizuri sana kupitia wimbo wake wa Jike Shupa aliomshirikisha mkali Ally Saleh Kiba ‘AliKiba’ ameeleza sababu ya kupotea kwenye muziki kwa takriban miaka miwili.
Kwenye makala haya, Nuh amefunguka mambo mengi yakiwemo ya kifamilia kama vile kulea mtoto wake mwenyewe:
Showbiz Xtra: Umekuwa kimya kwa muda mrefu kidogo, nini tatizo?
Nuh: Ni kweli kabisa nilikuwa kimya, lakini ni kwa sababu kuna vitu vingine nilikuwa nafanya ikiwemo na kusimamia studio yangu ambayo inaenda vizuri tu kwa sasa lakini pia nilifungua Pub yangu ambayo nilitakiwa niisimamie kwa ukaribu zaidi.
Showbiz Xtra: Kwa hivi sasa bado muziki unakulipa kama zamani au kuna kitu kingine unafanya?
Nuh: Muziki bado unanilipa sana, kwa sababu nina studio ambayo wanamuziki wengi wanakuja kurekodi. Nafanya matangazo kwenye studio yangu, hivyo hata kama niko kimya studio inafanya kazi vizuri sana na yote ni kwa sababu ya muziki wangu.
Showbiz Xtra: Unahisi ni kitu gani kimekurudisha nyuma kidogo kimuziki?
Nuh: Unajua sijarudi nyuma kabisa kimuziki kama nilivyo-sema hapo awali na ukimya wangu ulikuwa mzuri tu maana sasa hivi nina albamu tatu na nilikuwa zaidi nasimamia studio yangu.
Showbiz Xtra: Baada ya Jike Shupa, wimbo gani mwingine umeufanya ambao mkali?
Nuh: Unajua sio kila wimbo utakaoutoa utakuwa mkali, hapana lakini pamoja na hayo nimeachia wimbo mkali sana na Ben Paul na nyimbo zangu zinapigwa mpaka Tracy (TV ya Marekani), na ninaingia mpaka kumi bora huko na tayari imevuka nje ya Afrika maana hapa Afrika Mashariki najulikana vizuri tu.
Showbiz Xtra: Unahisi Shilole alikuwa akikubusti kwenye muziki wakati akiwa mpenzi wako?
Nuh: Hakuna mtu ambaye alinibusti kwenye muziki wangu hata siku moja zaidi ya Ma DJ na waandishi wa habari kwa sababu hao ndio waliofanya sauti yangu isikike, heshima natoa kwa niliowataja hapo juu.
Showbiz Xtra: Vipi kuhusu malezi ya mtoto wako uliyezaa na mkeo ambaye mmeshaachana kwa sasa, unaishi naye au yuko kwa mama yake?
Nuh: Naishi naye siku zote na mama yake anakuja kumuona tu akimmisi. Tayari tumeshambatiza na kumbadilisha dini. Anaishi maisha ambayo nilikuwa nayataka na yupo na mama yangu analelewa vizuri sana.
Showbiz Xtra: Mawasiliano yenu kwa sasa yapoje? Mmetengana kabisa na mzazi mwenzio?
Nuh: Mawasiliano yetu yapo vizuri kabisa kwa ajili ya mtoto tu na si vinginevyo. Yule ni mama, mtoto anahitaji upendo kwa pande zote mbili.
Showbiz Xtra: Vipi hufikirii tena kufanya kazi na Kiba?
Nuh: Ikitokea nitafanya naye maana yeye ni kama kaka yangu kabisa na ninamheshimu sana, naamini tutafanya tena na mashabiki wengi watafurahi.
Showbiz Xtra: Kutokuwa Wasafi Festival ni kwa ajili ya nyimbo yako ya Jike Shupa uliyofanya na Kiba au nini?
Nuh: Sijajua kwa nini maana kila mtu ana mipango yake na siku zote hakuna kitu kizuri kama msanii kupigiwa simu ya shoo na sio kuomba shoo lakini naamini hakuna shida kwa sababu pande zote mbili nafanya nao kazi pamoja na wanani-sapoti wote na wakati ukifika wataniita tu.
Showbiz Xtra: Vipi hujafikiria kuoa tena kwa ajili ya kumua-ngalia mwanao zaidi?
Nuh: Bado kwa sasa kuna vitu vingi nafanya kwa ajili ya mwanangu, wala sina haraka kwenye hilo.
Showbiz Xtra: Shukurani sana kwa muda wako.
Nuh: Nashukuru pia.
IMELDA MTEMA