The House of Favourite Newspapers

Omog Ampa Mkataba Mpya Juuko

0
Joseph Omog.

KOCHA Mkuu wa Simba, Joseph Omog, raia wa Cameroon, ameuelekeza uongozi wa timu hiyo umpe mkataba mpya wa kumbakisha klabuni hapo, beki wake kitasa, Juuko Murshid, raia wa Uganda, ikiwa ni muda mfupi baada ya wapinzani wao, Yanga, kumtolea macho kwa ajili ya kutaka kumsajili.

Mcameroon huyo ameyasema hayo wakati mkataba wa Juuko na Simba ukiwa umebakisha siku chache kabla ya kumalizika mwishoni mwa mwezi huu.

Chanzo kutoka ndani ya Simba kimeliambia Championi Jumatatu kuwa, Omog ameuambia uongozi umpatie mkataba mpya Juuko kutokana na kuwepo kwenye hesabu zake za msimu huu, pia anataka kumtumia kwenye michuano ya kimataifa ambayo Simba watashiriki.

“Kocha amependekeza kuwa lazima Juuko asainishwe mkataba mpya baada ya huu wa sasa wa miaka miwili kumalizika mwezi huu, taarifa ambazo tumesikia ni kuwa wapinzani wetu wanamnyemelea kwa ajili ya kumsajili.

“Unajua kuwa kocha amemjumuisha Juuko kwenye mipango yake ya muda mrefu ya kuwepo hapa ikiwemo kumtumia kwenye michuano ya kimataifa ambayo tutashiriki baadaye mwakani, lakini hata hivyo amekuwa mmoja wa walinzi wetu wazuri hivyo kocha amegoma kuuzwa.

“Lakini pia haiwezekani yeye kuruhusiwa kuondoka kwa sasa kwa sababu kuna uwezekano wa kumuacha Method Mwanjale, hivyo siyo rahisi kujikuta tumewaachia watu wawili wakati wamekuwa nguzo muhimu kwetu tangu msimu uliopita,” kilisema chanzo hicho ambacho kina wadhifa wa juu klabuni hapo.

Said Ally, Dar es Salaam.

Leave A Reply