The House of Favourite Newspapers

Penzini, kazini, nyumbani, kila kona stress, duh!

0
Attractive couple having an argument on couch at home in the living room
Attractive couple having an argument on couch at home in the living room

MPENZI msomaji karibu tena kwenye Jamvi la XXLove. Ni Jumatatu nyingine tena tumepewa kwa kudra za Mwenyezi Mungu kwa ajili ya kuelimishana juu ya uhusiano.

Kwenye mada ya leo tutajadili kuhusu mtu mwenye mpenzi aliyeshindwa kupata faraja kwa mwenza wake ambaye amevurugwa kazini na alitegemea akifika nyumbani mpenzi wake atakuwa faraja ya kumuondolea stress (msongo) lakini matokeo yake nyumbani nako kunakuwa ni mateso bila chuki.

Stress au msongo ni tatizo kubwa sana kwenye uhusiano wowote ule. Uwe wa kirafiki, kimapenzi na kadhalika. Msongo unaweza kuchangiwa na mambo mengi sana lakini kikubwa ni mtindo wa maisha ambao mtu, watu au jamii f’lani inaishi kwa maana ya ugumu na changamoto mbalimbali za kimaisha za kila siku, ingawa msongo wenyewe unaweza kuwa wa kusababishiwa au kujisababishia mwenyewe.

Ili kuondoa msongo, mhusika anatakiwa kukaa sehemu tulivu na kupumzika kwa muda ili kuondoa kilichomchanganya na kuingiza kitu kipya kabisa katika akili na mwili wake.

Najua unapata wakati mgumu sana unapoona mwenza wako ambaye ulitarajia angekuwa kimbilio, farijiko la moyo wako, furaha ya moyo wako, tabibu wa maradhi yanayokusibu kila siku, kila kukicha, kila mara naye anageuka stress kwako. Yaani ulitegemea kwa kuwa una stress za kazini basi ukifika nyumbani mpenzi wako atakuwa sehemu kubwa sana ya kukulainisha na kukuondolea stress lakini cha ajabu naye amekuwa sehemu ya kukuongezea stress. Pole!

Iko wapi furaha yako ya kuwa na mpenzi? Iko wapi raha ya kuwa na mtu kwa ajili ya kukufariji na kujiliwaza wakati unapokuwa umevurugwa? Yupo wapi mpenzi wako ambaye ulitegemea angekuwa msaada kwako unapokuwa umekwama kimaisha, kifikra, kimtazamo, kibinadamu na mengineyo?

Huoni furaha ya kuwa kwenye uhusiano maana ukiwa kazini ni stress, ukitoka unajua mpenzi wako nyumbani atakuondoa stress za kazini lakini cha ajabu anakuwa mtu wa kukuongezea!

Je, ni kweli huna bahati? Ni kweli ulikosea kuchagua mwenza wa kuishi naye? Ni kweli mpenzi uliyenaye si sahihi kwako? Kama siyo, yupi sasa ni sahihi na unawezaje kumjua? Je, utampata wapi? Kanisani, msibani, ngomani, gulioni, sokoni, shuleni, tamashani, shambani au sehemu gani? Kwa mtindo huo wa ‘kustresika’ kila sehemu, kila wakati, unawezaje kufanya faragha yako kuwa nzuri na bora? Unawezaje kumridhisha mpenzi wako ili afurahie tendo?

Bila shaka wewe ni mmoja wa wale ambao umewahi kukutana na suala hili na maumivu haya na ukaona kama vile huna bahati na mapenzi, basi unaweza kunitumia maoni yako nami nitayaweka hapa ili kupata suluhu ya pamoja.

Usikose kuhudhuria Semina ya Mimi na Uhusiano (M&U). Mada Kuu: KUNA MAISHA NJE YA MAUMIVU YA MAPENZI, itakayofanyika Agosti 27, mwaka huu kwenye Ukumbi wa Malaika, Kijitonyama, Dar. Kwa maelezo zaidi piga simu kwa namba 0657486745 au tembelea ukurasa wetu wa Mimi na Uhusiano kwenye Mtandao wa Facebook.

Leave A Reply