The House of Favourite Newspapers

PICHA CHAFU MITANDAONI, BABA PATTY ACHARUKA

 

DAR ES SALAAM: Baada ya kuvuja kwa picha zake ‘romantic’ akiwa na mwanamke mwingine tofauti na mkewe, mume wa muigizaji Rose Alphonce ‘Muna’, Peter Zacharia ameibuka na kumcharukia mkewe huyo akimtuhumu kumfanyia mchezo mchafu.

Picha hizo za Peter zimevuja siku tano baada ya mazishi ya mtoto wa Muna, Patrick kufanyika katika Makaburi ya Kinondoni jijini Dar, Jumamosi iliyopita.

 

TUJIUNGE NA PETER

Akizungumza na Risasi Mchanganyiko, Peter alidai kuwa anajua wazi anayezisambaza picha hizo mitandaoni ni Muna kwa nia ya kumchafua kwa sababu Aprili, mwaka huu alirudi nyumbani kwake Mwananyamala-Kisiwani na kujifanya kuwa anapanga vitu vyake ndani ya nyumba hiyo kumbe nia ni kunasa picha hizo.

“Unajua chochote kinachoendelea hivi sasa najua wazi ni mpango wa Muna, anajitahidi kuufanya ili mimi nionekane wa ajabu baada ya kuona watu walivyonichukulia tofauti kwenye kipindi chote cha msiba wa mtoto wetu hivyo anataka kunichafua lakini mimi kwa hilo sitetereki,” alisema Peter.

 

KUMBE MUNA ANAMJUA HUYO MWANAMKE

Akiendelea kuzungumza na Risasi Mchanganyiko kuhusiana na skendo ya kuvuja kwa picha hizo, Peter alimtaja mwanamke huyo kwa jina la Rehema. Alisema ni mwanamke ambaye Muna anamfahamu fika na alikuwa naye baada ya yeye (Muna) kutotulia nyumbani kwa muda mrefu.

“Kinachonishangaza mimi Muna anataka kujifanya huyo mwanamke ni mpya kwake lakini sio kabisa, anajua kila kitu na jinsi alivyokuwa akitangatanga kwa wanaume tofautitofauti, mimi ningeishi vipi kama mwanaume? Nafikiri anajua fika kwa kufanya hivyo atanichafua mimi kumbe anajichafua yeye,” alisema Peter.

 

ASEMA HATETEREKI

Akizidi kufunguka, Peter alisema kama mzazi mwenzake huyo anaona kufanya hivyo ni kumchafua, atakuwa anajisumbua maana yeye hata mshipa haumgongi kwa sababu anajua wazi akimaliza hilo la picha, hatakuwa na jipya lingine la kufanya.

“Jambo moja tu ambalo Muna alitambue ni kuwa mimi nipo imara sana, sitetereki na kitu chochote kile kwa sababu akimaliza kusambaza hizo picha atafanya nini tena cha kunichafua kama sio kujidhalilisha yeye mwenyewe?” alihoji Peter.

 

MUNA HAPATIKANI

Jitihada za kumpata Muna ili kumsikia anazungumziaje tuhuma hizo za kudaiwa kuhusika kuvuja kwa picha hizo za mumewe hazikuzaa matunda kufuatia simu yake kuita bila kupokelewa. Hata hivyo, Risasi Mchanganyiko linaendelea kumtafuta, akipatikana tutasikiliza pia kwa upande wake.

 

WATAALAMU WA MAMBO WAMTETEA MUNA

Hata hivyo, baadhi ya watu walio karibu na Peter wameweka bayana kuwa, huenda picha hizo akawa Muna hajazivujisha sababu hata huyo Rehema anaweza kuwa nazo hizo picha.

“Unajua anaweza kumhisi ni Muna kumbe ni Rehema maana Rehema mwenyewe naye huenda hajafurahia Peter kusema Muna bado ni mkewe siku ile pale msibani wakati yeye anajua kachukua nafasi, haya mambo bwana tuwaachie wenyewe,” alisema mtu huyo huku akiomba hifadhi ya jina.

 

Mtu huyo alizidi kueleza kuwa, mbali na Rehema, kuna uwezekano pia Peter akawa ameibiwa picha hizo na mtu mwingine maana siku hizi teknolojia imekua, unaweza kuweka chaji kwa mtu, picha zako zote zikahamia kwake. “Haya mambo siku hizi bwana ni hatari tupu, unaweza kuweka chaji kwenye kompyuta, picha zote zikahamia katika ile kompyuta,” alisema.

 

TUJIKUMBUSHE

Mgogoro wa Muna na mumewe ulijulikana hadharani hivi karibuni mara baada ya mtoto wao kipenzi Patrick kufariki nchini Kenya alipokuwa amekwenda kutibiwa.

Mara baada ya Patrick kufariki, mjadala mzito uliibuka mitandaoni ambapo kuna baadhi walisema baba yake ni Mtangazaji wa Clouds TV, Casto Dickson aliyewahi kuwa mpenzi wa Muna lakini wengine wakasema ni wa Peter.

 

Baada ya kuona hivyo, Peter aliibuka na kuweka wazi kuwa yeye ndio baba halisi wa Patrick kwa kuweka vithibitisho mbalimbali ikiwemo cheti cha ndoa na cheti cha kuzaliwa.

STORI: Mwandishi Wetu, Risasi Mchanganyiko.

Comments are closed.