PSSSF Yawanoa Jeshi la Polisi Tanzania Jinsi ya Kuwasilisha Nyaraka Kidijitali

MFUKO wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umeendesha mafunzo ya namna ya kuwasilisha madai kupitia mifumo ya TEHAMA kwa maafisa wa Dawati la Mafao wa Jeshi la Polisi Tanzania.
Akizungumza na maafisa hao jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF Bw. Abdul-Razaq Badru, amesema, kwa sasa PSSSF imejikita katika kutoa huduma zake kwa njia ya TEHAMA ili kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wanachama na wadau.
“Kisheria tumepewa jukumu la kusimamia masuala ya pensheni kwa watumishi wa umma na Jeshi la Polisi ni moja kati ya makundi maalum yanayohudumiwa na PSSSF. Kwa kutumia huduma zetu za kidijitali, tunajitahidi kutoa huduma sahihi na kurahisisha mnyororo wa utoaji huduma.”

Akieleza jinsi PSSSF inavyokwenda na usasa, Bw. Badru alibainisha kuwa PSSSF imeanzisha huduma mbalimbali za mifumo ya kidijitali ikiwemo PSSSF Kiganjani, ambapo mwanachama anaweza kujihudumia mwenyewe ikiwa ni pamoja na wastaafu kujihakiki kupitia simu janja mahali popote bila ya uhitaji wa kufika kwenye ofisi za PSSSF.
Naye Mkurugenzi wa Uendeshaji, Bw. Mbarouk Magawa, alisema Mafunzo kwa maafisa wa Polisi yanakusudia kuleta ufanisi na uwazi katika kudai mafao kupitia njia za kidijitali.

“Hii ni hatua muhimu katika kuhakikisha wanachama wanapokea mafao yao kwa wakati na kwa ufanisi.” Alisisitiza.
Awali Kamishna wa Utawala na Menejimenti ya Rasilimali Watu wa Jeshi la Polisi, CP Suzan Kaganda, akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Camillius Wambura, alisema hatua hiyo ni muendelezo wa utekelezaji kwa vitendo wa maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliyotoa Septemba 2024, wakati wa Mkutano Mkuu wa Makamanda na Wakuu wa Vikosi wa Jeshi la Polisi, kuhusu matumizi ya TEHAMA kwenye Utendaji wa Jeshi hilo.
CP Kaganda amewahimiza maafisa hao kutumia fursa hii ya kipekee, kuwa wepesi kujifunza ili waweze kwenda na kasi ya mabadiliko ya teknolojia.
“Mfumo wa kuwasilisha madai kupitia mtandao utasaidia wanachama kufuatilia madai yao wenyewe kwa haraka na kwa uwazi.” Alisisitiza.



