The House of Favourite Newspapers

Puma Yampa Makonda Tsh 40m za Upasuaji Moyo kwa Watoto


Kampeni ya Matibabu ya Upasuaji wa Moyo kwa Watoto 10 kutoka familia duni kila mwezi kwa Muda wa Miezi 6 iliyoanzisha na Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Paul Makonda imeendelea kuleta matokeo chanya na kuokoa Maisha ya Watoto ambapo leo Septemba 30 Kampuni ya Mafuta ya Puma Energy imemkabidhi Mkuu huyo wa Mkoa hundi ya shilingi Milioni 40 ikiwa ni sehemu ya Kuunga mkono kampeni hiyo.

 

Akipokea hundi hiyo RC Makonda amesema kiasi hicho cha fedha kitasaidia kuokoa maisha ya takribani watoto 20 kutoka familia Duni ambao wamelazwa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete wakisumbuliwa na tatizo la moyo lakini wameshindwa kupata matibabu kutokana na kushindwa kumudu gharama.

 

 

RC Makonda ameeleza kuwa alikutana na Mkurugenzi wa Kampuni ya Puma kwenye Hafla ya Ugeni wa Maraisi wa Nchi za SADC iliyofanyika Ikulu na katika hafla hiyo mkurugenzi huyo alijisogeza kwa RC Makonda kwa lengo la kujitambulisha ambapo Mkuu wa Mkoa alitumia nafasi hiyo kumuelezea Changamoto ya uwepo wa Watoto zaidi ya 500 wenye tatizo la moyo na mkurugenzi huyo alipokea kwa mikono miwili ombi hilo na hatimae leo amekabidhi hundi.

 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kampuni ya Puma Energy Bw. Dominic Dhanah amesema kampuni hiyo itaendelea kuunga mkono juhudi za RC Makonda katika masuala mbalimbali yanayolenga kutatua kero za Wananchi wasiojiweza.

 

 

Hayo yote yamejiri wakati wa Hafla ya kufunga mafunzo ya Usalama barabarani kwa wanafunzi zaidi ya 20,000 kutoka shule 9 za mkoa wa Dar es salaam yaliyotolewa na Taasisi ya AMEND na kudhaminiwa na Kampuni ya Puma Energy ambapo RC Makonda amewataka Madereva kuzingatia Sheria, kanuni na taratibu za Usalama Barabarani ili kuepusha ajali kwa watembea kwa miguu.

Comments are closed.