The House of Favourite Newspapers

PUTIN ASEMA: SIJAWAHI KUWA NA ‘SMARTPHONE’

Rais wa Russia, Vladimir Putin (kulia) aliyekiri hana simu ya kisasa (smartphone).
Kiongozi huyo aliyewahi kuongoza pia shirika la ujasusi la Urusi ya Kisoviet (KGB) amesema huwatumia wasaidizi wake kumtafutia habari anazotaka.

“SINA simu ya smartphone,” ndivyo ambavyo husema Rais wa Russia, Vladimir Putin, kila anapoulizwa iwapo ana simu hizo za kisasa.

 

Licha ya kuambiwa kwamba “kila mtu ana smartphone mfukoni”  huko Siberia, nchini Russia, wakati akiwa ziarani, kiongozi huyo pia aliwahi kusema kwamba hataki kutumia tovuti (website) na aliwahi kukiri kwamba mtandao wa Internet ni kimradi cha shirika la ujasusi la Marekani – CIA – na kwamba nusu ya kazi yake ni kuonyesha ngono.

 

Pamoja na kwamba watu wengi nchini mwake, wakiwemo wanafunzi,  huchakarika ili kupata aina hizo za simu, Putin amefichua kwamba analitawala taifa hilo la watu milioni 144 bila kutumia smartphone.

 

Akiwa amekiri pia kwamba hapendi mambo ya technolojia mpya, amesema kamwe huwa hatumii Internet na kama ikilazimika, huwatumia wasaidizi wake kumtafutia kitu anachokitaka.

 

Putin mwenye umri wa miaka 65, alithibitisha kutopenda kwake masuala ya mitandao (apps) alipokutana na wanasayansi na wasomi huko Siberia ambako mkuu wa kituo cha uafiti wa zana za nyuklia, Kurchatov alimwambia kwamba “kila mtu ana smartphone mfukoni”.

 

Amesema pia kwamba hapendi kujiunga katika mitandao ya kijamii, kinyume na mwenzake wa Marekani, Rais Donald Trump, anayetumia mtandao wa Twitter kama silaha yake binafsi ya kisiasa.

 

Mwaka jana alipokutana na watoto wa shule, Putin aliulizwa iwapo huwa anatazama mtandao wa Instagram au mitandao mingine ya kijamii wakati wake wa mapumziko, naye akasema: “Mimi binafsi situmii kitu hiki.  Huwa nafanya kazi kubwa hadi usiku, sina muda wa Instagram.”

 

Kauli hizo za Putin zimekuja wakati kuna ripoti kwamba wadukuaji wa mitandao wa Russia wanajaribu kuhujumu chaguzi katika nchi za kidemokrasia za Magharibi.

 

WALUSANGA NDAKI/MITANDAO/MASHIRIKA YA HABARI

 

Comments are closed.