The House of Favourite Newspapers

Q-Chillah, Ray C, TID, Matonya, Marlaw na Besta Turudisheni Muziki Wetu

0

Stori: BRIGHTON MASALU | RISASI JUMATANO | RISASI VIBES

NINACHO-KIPATA, nagawana na wenzangu maskini zaidi yangu, wenye dhiki kama mimi, waliopoteza wazazi wao kwa ugonjwa wa Ukimwi… wale wenzangu na mimi wasiojiweza kitandani, yaani wa leo wa kesho, dua nawaombea… moyo wangu wa mbigili… kila mtu wamchoma….”

“Hebu tathmini kisha nipe jibu…,hivi kwa nini hutaki kunijibu, mitihani yote nimeshinda…nadhani ni wakati penzi letu sisi liwe wazi, roho yangu inauma…maumivu sasa basi…Sasa basi, niko thabiti, nielewe pesa siyo mapenzi, kwa utenzi huu nielewe baby, nakuhitaji mpenzi, wewe ndiyo faraja yangu…”

TID

“Umenikataa bila sababu, umeninyanyasa bila aibu… nimepata mwingine tabibu sasa wanifuatafuata nini?

Kama ni pendo langu nilikupa lote, nilikujali kwa kila kitu na kukupa mahaba yote, sikudhani ungenidharau na kuniletea wengine…sikudhani ungenigeuka na kuanza kuninyanyasa, pesa na magari yako yalikufanya uwe kiburi, uliniacha ukaenda zako na kusahau utu wangu, penzi langu hukuthamini…, ukaniacha na majonzi, nimebadilika nini wanifuata mimi wa nini…?”

“Na taarifa ikaja kwako wewe Ritha…, uende Arusha nduguzo wanakuita ukani-kiss mimi na mtoto, nikaku-kiss…, Kurudi Iringa uishi nami ndugu zako wamekuzuia… ila ukapiga simu mume wangu nakuja, na maneno ya konda kwenye basi ulifika akakupa siti, ulipokaa ukakaa… ile siku mimi nimelewa, niko mimi na mwanangu kumpokea mke wangu, konda akasema si wewe ila tu ni mwili wakooo…”

Ray C

Nimelazimika kuanza na baadhi ya mashairi ya nyimbo zenu kadhaa ambazo zilishika na kuteka hisia za wadau wengi wa burudani, ili niweke kumbukumbu sawa namna ambavyo ubora wa kazi zenu utabaki kama alama nzuri kabisa kwenye anga la muziki wetu.

Nimeanza na baadhi ya mashairi ya Wimbo wa Ninachokipata wa Q- Chillah, nikagusia tungo ya Wimbo wa Nyota Yako wa TID, nimekumbushia uhondo wa sauti ya Ray C kisha nikavuta fikra kwenye Wimbo wa Ritha wa Marlaw. Kama nafasi ingetosha, ningeweka pia ya Kati Yetu ya Besta na Anita ya Matonya.

Hadi sasa tunao wasanii wengi mno, ambapo ni dhahiri wanajitosheleza kukonga nyoyo zetu linapokuja suala la burudani, ingawa si kwa kiwango ambacho ninyi mlitufikisha. Nataka niseme wazi kuwa, ninyi ni kati ya wasanii wachache ambao historia ya muziki wetu haitaacha kuwataja kwa wakati wowote.

Q- Chillah

Q- Chillah, sauti yako ni adhimu mno. Inajua kutembea na biti huku ikigusa hisia za ndani kabisa. Unajua kuimba na hata muziki wenyewe unajua kuwa unajua kuutendea haki. Maiki huwa

 inakutii kila ukiikamata na hata head phones, hutulia kabisa unapokuwa studio ukifanya mambo. Uko wapi kaka? Zile tungo za Tutaonana wabaya ziko wapi?

Braza TID nakumbuka enzi na nyakati za Zeze, Nyota Yako na tungo nyingi ambazo zilionesha ushababi wako. Makeke yako kwenye uchezaji na mikogo katika kuwakilisha ujumbe kwenye video, zilikonga na kushika hisia zetu kwa kiwango kisichotamkwa kaka. Uko wapi? Mbona siuoni ule utundu wa Nilikataa uliyofanya na Q-Chillah? Ujuzi na utaalam wa kucheza na mistari kama ulivyowakilisha vyema kwenye ngoma ya Asha umeenda wapi?

Marlaw

Marlaw, nakumbuka sana mtiririko wa ngoma ya Ritha. Uligusa na kuumiza wengi kwa namna ambavyo uliimba kwa hisia, ikafika hatua baadhi ya watu kuamini kuwa ile ni simulizi ya kweli iliyowahi kukutokea maishani mwako. Mbona kimya tena kaka? Unakumbuka kazi zako kama Pipi? Vipi kuhusu Busu la Pinki?

Besta, ngoma yako ya Kati Yetu iligeuka lulu ndani na nje ya nchi! Ujio wako kwenye ulingo wa sanaa ya muziki ulipokelewa kama faraja bora kabisa, uliongeza idadi ya wanamuziki wa kike, hakika tulikupokea kwa shangwe na mikono yetu yote, lakini ulipoolewa tu umepotea jumla, kwa nini?

Matonya

Matonya, hakuna mwenye sauti ya kulalamika kama wewe kaka. Mashairi uliyoyatiririsha kwenye ngoma kama Vaileth, Spea Tairi na Anitha hadi leo yametengeneza makazi ya kudumu kwenye kuta za bongo zetu, umepotelea wapi?

Najua maisha yana mikikimikiki mingi mno. Huenda mna kazi zilizowafanya mkose muda wa kufanya muziki, lakini mjue mlituonjesha ladha ambazo kwenye muziki tunaousikia sasa hivi hazipo tena. Simaanishi kuwa hakuna wanamuziki wenye uwezo kama wenu, wapo wengi na huenda wana ubunifu kuliko ninyi lakini ninachomaanisha hapa ni upekee wenu.

Mmejaribu kurudi mara kadhaa kwa nyakati tofauti, lakini si kwa namna ambavyo mlituteka. Kila mmoja wenu kwa wakati wake, akae na atafakari namna alivyoweza kushika soko la muziki kwa kazi nzuri na jinsi ambavyo atarejea tena. Wapo vijana wanafanya vizuri sana lakini hawajaziba pengo la kazi zenu.

Ndimi Mjenzi wa Taifa kupitia Kalamu (MTK), Brighton Masalu, 0673 42 38 45

 

Mauaji Ya Kiongozi Wa CCM Kibiti Mke Asimulia Mumewe Alivyouawa

Leave A Reply