KOREA Kaskazini imesema haioni manufaa ya majadiliano kati yake na Marekani, hadi Marekani isitishe kile ilichokiita hatua za uhasama za kijeshi dhidi ya Korea.
Kauli hiyo imefuatia wakati mjumbe wa Marekani akizuru Korea Kusini kwa lengo la kufufua mazungumzo ya nyuklia na Pyongyang.
Mazungumzo kati ya Pyongyang na Washington yamekwama, tangu mkutano wa pili wa kilele kati ya Rais wa Marekani, Donald Trump, na kiongozi wa Korea Kaskazini, Kim Jong Un, mjini Hanoi, Vietnam, Februari, ulipovunjika bila makubaliano.
Wawili hao walikutana tena mwezi Juni katika ukanda wa amani kati ya Korea mbili na kukubaliana kuanzisha tena majadliano ya ngazi ya kikazi, lakini mazungumzo hayo bado kuanza.
Wakati huohuo, Korea Kaskazini imefanya majaribio kadhaa ya makombora ya masafa mafupi katika wiki za karibuni, kupinga mazoezi ya kijeshi ya kila mwaka kati ya Marekani na Korea Kusini, ambazo inayaona kama mazoezi ya kujiandaa na uvamizi.
Stephen Biegum, mjumbe maalumu wa Marekani kwa ajili ya Korea Kaskazini, anayeongoza mazungumzo ya kikazi, aliwasili mjini Seoul Jumanne jioni kwa ziara ya siku tatu, na alisema Washington itakuwa tayari kushiriki mazungumzo mara itakaposikia kauli kutoka Pyongyang.
Comments are closed.