RAIS John Magufuli leo tarehe 28 Februari, 2020, amekagua maendeleo ya ujenzi wa msikiti wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) unaojengwa Kinondoni Jijini Dar es Salaam.
Msikiti huo unajengwa kwa ufadhili wa Mfalme Mohammed VI wa Morocco baada ya kuombwa na Rais Magufuli alipofanya ziara rasmi hapa nchini Oktoba 2016.
Akiongozwa na Mufti wa Tanzania, Sheikh Aboubakar Zubeir bin Ally, Magufuli amejionea kazi za ukamilishaji wa jengo jipya la msikiti na jengo la ofisi ya Taasisi ya Mfalme Mohammed VI wa Morocco zikiendelea kukamilishwa, na ameelezea kufurahishwa kwake na ubora na uzuri wa msikiti huo.
Magufuli amemshukuru Mfalme Mohammed VI wa Morocco kwa kutekeleza ombi alilomuomba la kuwajengea Waislamu msikiti mkubwa kuliko yote hapa nchini, na amempongeza Mufti wa Tanzania na Waislamu wote kwa kujengewa nyumba nzuri ya ibada.
Mufti amemshukuru Magufuli kwa kuwajali Waislamu na kuwaombea msaada wa kujengewa msikiti huo ambao ujenzi wake umefikia asilimia 97.
Akiwa na viongozi wenzake wa BAKWATA, mufti ameongoza dua ya kumuombea Magufuli na taifa ili Mwenyezi Mungu aiepushe Tanzania dhidi ya maradhi ya homa ya virusi vya corona, kudumisha amani na utulivu na kuombea uchaguzi mkuu utakaofanyika baadaye mwaka huu ufanyike vizuri na kwa amani.