The House of Favourite Newspapers

Rais Magufuli afuta sherehe za maadhimisho ya Ukimwi

0

maggufulii

Rais Dk. John Pombe Magufuli.

Rais John Magufuli amesitisha maadhimisho ya siku ya Ukimwi kitaifa ambayo yalikuwa yafunguliwe mkoani Singida jana na kufikia kilele chake Desemba mosi mwaka huu mjini humo.

Badala yake Rais Dk Magufuli ameagiza fedha zote ambazo zilitengwa na serikali pamoja na wahisani mbalimbali kwaajili ya maadhimisho hayo zielekezwe kununua dawa kwaajili ya waathirika wa Ukimwi na vitendanishi.

Akizungumza na moja kwa moja na Televisheni ya Taifa (TBC), Mwenyekiti Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS), Dk Fatma Mrisho, amesema serikali imetoa agizo hilo jana wakati tayari mkuu wa Mkoa wa Singida akiwa ameshafungua maonesho ya maadhimisho hayo.

“Serikali imesitisha maadhimisho ya mwaka huu Singida na badala yake fedha zilizopangwa kwaajili ya maadhimisho ziende zikanunue dawa za virusi vya Ukimwi, dawa za kudhibiti maambukizi ya ukimwi na vitenganishi,” amesema Mrisho.

Dk Mrisho amesema kuwa tayari taarifa za kusitisha maadhimisho hayo zimesha wafikia washiriki na wale walio kuwa njiani kuelekea Singida wamegeuza.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Dar es Salaam juzi kabla ya sherehe hizo kusitishwa, Mwenyekiti Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS), Dk Fatma Mrisho alisema maadhimisho ya mwaka huu yalikuwa yatanguliwe na maonesho ya wadau yatakayojumuisha huduma mbalimbali zikiwamo za utoaji elimu na burudani.

Dk Mrisho alisema huduma nyingine zilizopangwa kutolewa katika maadhimisho hayo ya wiki moja ni upimaji wa hiari wa watu zaidi ya 3,500 wanaoishi na virusi vya Ukimwi na utoaji ushauri nasaha, upimaji wa shingo ya uzazi, sukari, uzito, damu na kupata elimu itakayotolewa kupitia vikundi vya sanaa na burudani.

Maadhimisho ya mwaka huu yanachagizwa na kaulimbiu ya ‘Tanzania bila maambukizi mapya ya VVU, vifo vitokanavyo na Ukimwi na ubaguzi na unyanyapaa inazewekana.’

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dk Parseko Kone aliwaambia waandishi wa habari ofisini kwake hivi karibuni kuwa maadhimisho hayo yanatarajiwa kuanza Novemba 24 mwaka huu kwenye viwanja vya Peoples Club ambapo uzinduzi utakuwa Novemba 25 kabla ya kilele, Desemba mosi.

Hii ni mara ya tatu tangu Rais Dk Magufuli aingie madarakani kuzuia maadhimisho yanayogharimu fedha nyingi za sherehe na fedha zake kuelekeza ikanunulie vifaa tiba mahospitalini.

Awali Rais aliagiza fedha zilizotengwa kwaajili ya hafla ya uzinduzi wa Bunge zaidi ya shilingi Milioni 225 ziende kununulia vitanda vya hospitali ya taifa Muhimbili.

Aidha Rais pia alisitisha maadhimisho ya siku ya Uhuru Desemba tisa mwaka huu na badala yake watu wafanye kazi katika maeneo yao ya kazi hasa usafi wa mazingira.

Leave A Reply