Rais Samia Aandika Historia Mpya Katika Sekta ya Uvuvi Nchini (Picha +Video)
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan leo Septemba 19, 2023 ameandika historia mpya katika sekta ya uvuvi nchini, baada ya kuweka jiwe la msingi kuashiria uzinduzi wa ujenzi wa bandari ya uvuvi ya Kilwa Masoko mkoni Lindi.
Badari hiyo inayotajwa kama ya kisasa na kipekee kuwahi kujengwa nchini tangu uhuru, ikikamilika, itawezesha meli za uvuvi zinazovua katika ukanda wa uchumi wa Bahari ya Tanzania na Bahari Kuu, kutia nanga na kushusha samaki wanaolengwa na wale wasiolengwa kwa ajili ya soko la ndani na nje ya nchi.
Aidha, uwepo wa bandari hiyo, utachochea uwekezaji katika ujenzi wa viwanda vya kuchakata samaki na miundombinu ya uhifadhi wa mazao ya uvuvi. Hivyo, uwekezaji huu, unaenda kuimarisha biashara ya mazao ya uvuvi kwenda nje ya nchi kutoka tani 40,721.53 zenye thamani ya Dola za Marekani Milioni 249.54 hadi tani 52,937.99 na kuchangia takriban asilimia 10 katika pato la Taifa ifikapo mwaka 2036.
Bandari hiyo pia inatarajiwa kutengeneza ajira kwa watanzania takriban 30,000 huku katika hatua za awali za ujenzi, jumla ya ajira za muda mfupi 278 zimetolewa ambapo kati ya hizo ajira 106 sawa na asilimia 38 zimetolewa kwa wakazi wa wilaya za Mkoa wa Lindi.
Pamoja na uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa bandari ya Uvuvi, Rais Samia pia amegawa boti 34 kati ya boti 160 ambazo zinatolewa nchi nzima. Boti hizi kwa ukanda wa bahari ya Hindi zipo 92 zikihusisha wavuvi na wakulima wa mwani.
“‘Serikali imejipanga kuhakikisha mazingira ya wavuvi na wakuzaji viumbe maji yanaimarika ndio maana leo nimegawa boti za kisasa zikiwa na kifaa cha kuonyesha upatikanaji wa samaki na uhifadhi wa samaki,’ amesema Rais Samia.