The House of Favourite Newspapers

Rais Akubali Mwanaye Auawe Kisa Madawa ya Kulevya

0
Rais wa Ufilipino, Rodrigo Deterte.

RAIS wa Ufilipino, Rodrigo Deterte, amesema yuko tayari mwanawe auawe iwapo madai kwamba anahusika katika biashara ya madawa ya kulevya yatakuwa ya kweli. Ameongeza kwamba polisi ambao wataendesha mauaji hayo watalindwa dhidi ya kufunguliwa mashitaka.

Paolo Duterte mwenye umri wa miaka 42, alifikishwa mbele ya jopo la maseneta alipokana madai yaliyotolewa na wabunge wa upande wa wapinzani kwamba alikuwa mwanachama wa kundi la Wachina lililosaidia kuingiza ndani ya nchi hiyo madawa ya kulevya aina ya ‘crystal methamphetamine’.

Mtoto wa Rais Deterte, Paolo Duterte (kushoto) akiwa mahakamani na mtuhumiwa mwenzake.

Rais Duterte hakumaanisha hasa madai hayo dhidi ya mwanaye, lakini alisisitiza maneno yake aliyoyasema wakati wa kampeni ya uchaguzi mwaka jana kwamba hakuna mwanaye yeyote anayejihusisha na madawa ya kulevya, lakini wangekabiliwa na adhabu ngumu zaidi iwapo wangefanya hivyo. “Kama nina watoto wanaojihusisha na madawa ya kulevya, waueni ili watu wasiwe na la kusema,” alisema Duterte katika hotuba yake aliyoitoa juzi (Jumatano) usiku mbele ya wafanyakazi wa serikali katika ikulu ya Manila.

Paolo Duterte.

“Hivyo, nilimwambia Pulong (jina la utani la Paolo) kwamba amri yangu ni kukuua iwapo utakamatwa. Na nitawalinda polisi watakaokuua, kama ni kweli ujajihusisha na mambo hayo,” alisema.

Duterte (72) alishinda uchaguzi wa rais kwa kampeni kali aliyoendesha akiahidi kuyatokomeza madawa katika jamii kwa kuua wauaji na watumiaji wa madawa hayo wapatao 100,000.

Tangu ashike madaraka katikati ya mwaka jana, polisi wameripoti kuua watu zaidi ya 3,800 katika oparesheni dhidi ya madawa ya kulevya wakati maelfu wameuawa katika mazingira yasiyoelezeka. Maelfu ya wakosoaji na wafuasi wake, walifanya mikutano mbalimbali jana (Alhamisi) kujadili vita hiyo kali ya mauaji na vitisho vya kijeshi mitaani.

Leave A Reply