TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetangaza kuanzia Februari 14 hadi 20, 2020, uhuishwaji wa Daftari la kudumu la Wapiga Kura Jijini Dar es Salaam utaanza, ambapo kutakuwa na vituo 1661 ikiwa vimeongezeka vituo vipya 47 kwa ajili ya zoezi hilo.
Hayo yamesemwa leo Jumanne, Februari 11, 2020, na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda wakati akitoa salam za Mkoa wa Dar kwa Rais John Magufuli alipokuwa akizindua wilaya mpya ya Kigamboni.
“Ninawasihi wananchi wote wa Mkoa wa Dar es Salaam ifikapo Februari 14, ambayo inafahamika kama siku ya wapendanao twendeni tukajiandikishe na kuhakiki taarifa zetu tuonyeshe upendo wetu kwa maendeleo na hapo ndipo tutapata sifa stahiki ya kumchagua kiongozi wetu.
“Bila kuwa na haki ya kupiga kura utapoteza haki yako na mwisho wa siku utabaki kulalamika, tunahitaji tumchague kiongozi wetu tena aweze kuendeleza yale mema mazuri aliyoyafanya kwa ajili ya mstakabali mkubwa wa taifa letu kwa ajili ya kizazi chetu na kizazi kijacho.
“Sisi Afrika Mashariki na Central Africa tukiweka hub (kituo) yetu ya magari Kigamboni watu watatoka Afrika zote kuja kununua magari Kigamboni. Uchumi wetu utakua, hoteli zetu zitafanya kazi nzuri na wana Kigamboni hapa watabaki kuteleza tu.
“Lakini moja kubwa umenipa jukumu la kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam na nisingependa kuongea mengi kwa sababu nawafahamu wananchi wa Dar es Salaam, ukiwaambia mambo mengi wanasahau. Nataka leo tujikite katika Wilaya moja ya Kigamboni,” amesema Makonda.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Manispaa ya Kigamboni, Ludigija Ng’wilabuzu, amesema: Umetupatia Bilioni 4.3 kwa ajili ya jengo la Manispaa ya Kigamboni lenye uwezo wa kuchukua watumishi 450. Tumepokea Bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya, majengo yako saba na yote yamekamilika.
Pia tulipatiwa shilingi Milioni 800 kwa ajili ya upanuzi wa vituo viwili vya afya vya Kigamboni na Kimbiji, majengo yamekamilika na huduma zinaendelea. Mwaka 2018/19 Elimu Sekondari tulipokea shilingi Bilioni 2 ya ujenzi wa madarasa na maabara, Manispaa hii haikuwa na masomo ya kidato cha 5 na 6, sasahivi wanafunzi wameanza masomo.
Aidha, Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, Sarah Msafiri, amesema: “Wananchi wa eneo hili walikuwa wanatembea umbali mrefu sana kufika kwa Mkuu wa Wilaya, Mkurugenzi na Taasisi zingine, leo hii wananchi wanapata huduma zote sehemu moja.”
“Tuna mradi wa umeme wa dege wa Bilioni 26 ambapo mradi wa maji wa visima vinane wa Kimbiji vimekamilika, DAWASA wanajenga tenki kubwa na kusambaza maji kwa kilomita 65,” amesema.