The House of Favourite Newspapers

Ruby Alia Kutupiwa Vitu Nje, Aomba Msaada wa Wanasheria

AMA kweli penzi likiisha ni kama shubiri! Mwanamuziki mahiri wa Bongo Fleva, Hellen George ‘Ruby’ amesema kuwa, mwanaume ambaye alimpenda na kumthamini, hakuwa mwanaume bali ni nyoka. 

 

Ruby amesema mwanaume huyo aitwaye Kusah amemsababishia aibu ya kutupiwa vyombo nje na baba mwenye nyumba aliyokuwa anaishi maeneo ya Mbezi-Salasala jijini Dar.

Kikizungumza na Gazeti la Ijumaa Wikienda, chanzo chetu makini kilisema kuwa, nyumba aliyokuwa amepanga Ruby na mwanaume wake huyo, kila siku ilikuwa ni ugomvi na mara nyingi walikuwa wakisumbua kulipa kodi.

 

“Ruby na Kusah wamekuwa ni watu wa kugombana kila kukicha kiasi ambacho watu walikuwa wakigombelezea, maana huyo mwanaume alikuwa akitoa kipigo kikali bila kujua kuwa wana mtoto mmoja,” alisema mnyetishaji huyo ambaye ni jirani yao.

Chanzo hicho kiliendelea kutiririka kuwa, siku ya tukio, Ruby alikuwa amelala ambapo Kusah aliingia na kuchukua simu ya msanii, ndipo akakutana na meseji ya msanii Jux. “Alichokifanya ni kumpiga ngumi ya shingo, kisha kumshushia kipigo kikali kilichomfanya Rubby akimbilie kwa rafiki yake akiwa pekupeku huku chumba chote kikitapakaa damu.

 

“Kama ni kipigo tu, basi Ruby amekipata. Lakini hiki cha hivi karibuni kilikuwa ni hatari. “Kibaya zaidi, wakati wanagombana walikuwa wanadaiwa kodi ya shilingi laki saba, hivyo baba mwenye nyumba akawatupia virago vyao nje,” kilisema chanzo hicho.

 

Ijumaa Wikienda lilizungumza na Ruby ambaye alisema amepitia kipindi kigumu mno kwenye maisha yake ya kimapenzi na huyo mzazi mwenzake, kwani alikuwa akiishi kwenye kipigo kikali kila siku bila sababu za msingi.

“Nimejiuliza maswali mengi sana kwa nini nikubali kipigo na mimi bado ni mdogo? “Nimeamua kuachana naye na simtaki kabisa. Ni kweli hivyo vitu vilivyotolewa nje kwa sababu yeye ndiye aliyesababisha yote hayo, kwani ndiye aliyetakiwa kulipa, matokeo yake nimeambulia aibu na fedheha,” alisema Ruby akiomba wanasheria kuingilia kati kusaidia wanawake wanaopigwa na wanaume.

 

Kwa mujibu wa Ruby, aliamua kumsaidia baba watoto wake hasa kwenye eneo la kutoboa kimuziki kwa kumuunganisha na mastaa wakubwa kama Diamond na Jux, lakini mwisho wa siku jamaa huyo aliishia kumtusi na kumwambia kuwa anatembea nao, jambo ambalo siyo kweli.

STORI: IMELDA MTEMA, DAR

Comments are closed.