Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) imewafikisha mahakamani, mmiliki kampuni ya PAP, Habirnder Seth Singh na mfanyabiashara James Rugemalira kwa makosa ya uhujumu uchumi.
Akizungumza na waandishi wa habari, leo Jumatatu, Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Kamishna Valentino Mlowola amesema, “Leo nawapa taarifa kuwa tunawafikisha mahakamani watuhumiwa wawili, kwa makosa ya kuhujumu uchumi na mengine yanayofanana na hayo.”
Amesema kwa muda mrefu amekuwa akiulizwa kesi za Escrow na kampuni ya kufua umeme ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL) zimeishia wapi, hivyo taasisi hiyo imechunguza shauri hilo kwa muda mrefu na kujiridhisha kwamba linaweza kufikishwa mahakamani.
“Kwa hatua ya awali wataenda Mahakama ya Kisutu, baada ya hapo kuna utaratibu wa kimahakama, watapelekwa mahakama maalumu kutokana na kiwango cha hujuma kilichofanyika na fedha zilizohusika,” amesema Mlowola.
Kwa mujibu wa wakili wa watuhumiwa hao, Onesemo Mpinzile ameeleza kuwa washtakiwa wamesomewa mashtaka sita likiwemo la uhujumu uchumi.
“Kwa misingi ya kisheria, washtakiwa wamenyimwa dhamana na kurudishwa rumande hadi Julai 3, mwaka huu, huku upelelezi ukiendelea.
“Mawakili tutakaa kuona namna gani tutawasilisha rufaa yetu kwa kuwa Mahakama ya Kisutu imesema haina mamla kisheria ya kutoa dhamana kwa washtakiwa hao,” alisema Mpinzile.
PICHA ZOTE NA RICHARD BUKOS | GLOBAL TV ONLINE