Ruvu Shooting: Lazima Tuwachape Namungo
OFISA Habari wa Ruvu Shooting, Masau Bwire, amefunguka kuwa, wamejipanga kuchukua pointi tatu dhidi ya Namungo FC katika mchezo wao unaotarajiwa kupigwa Julai 14, mwaka huu kwenye Uwanja wa Mabatini, Pwani.
Ikiwa nafasi ya 10 kwenye msimamo wa Ligi Kuu Bara, Ruvu Shooting imekusanya pointi 38 katika michezo 32, huku ikishinda 10, imepoteza 14 na sare nane.
Akizungumza na Spoti Xtra, Bwire alisema maandalizi ya mechi zao mbili zilizosalia yanaendelea vizuri, lakini wamejikita zaidi katika mechi ijayo dhidi ya Namungo.
“Maandalizi yanaendelea kama kawaida na tupo tayari kwa mechi muda wowote, tumejipanga kuhakikisha hachomoki mtu katika mechi hizo lazima tuchukue pointi zote dhidi ya wapinzani wetu.
“Tunafahamu hakuna mechi rahisi kwenye soka, hivyo ni wazi huu mchezo utakuwa mgumu kwa sababu kila mtu anataka hizo pointi ili iweze kuwa salama kwa upande wake, lakini na sisi kwa upande wetu tumejipanga vizuri sana,” alisema Bwire.
Baada ya mchezo huo, Julai 18, mwaka huu, Ruvu Shooting itamaliza msimu uwanja wa nyumbani kwa kucheza dhidi ya Azam.
HAWA ABOUBAKHARI, Dar es Salaam