WANAFUNZI watano wa shule ya msingi Ndelenyuma, Ruvuma, waliofariki dunia na mmoja kujeruhiwa baada ya kugongwa na Land Cruiser juzi Februari 12, 2020, lililokuwa likitokea Songea kwenda Madaba, wamezikwa jana katika makaburi ya Kijiji cha Ndelenyuma, Halmashauri ya Madaba mkoani Ruvuma.
Maziko hayo yalihudhuriwa pia na Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christina Mndeme.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo, Simon Maigwa, alisema ajali hiyo ilihusisha gari ndogo iliyokuwa na watu wawili waliokuwa wanakwenda kufanya ukarabati wa mnara.
“Wanafunzi sita waligongwa, watano walikufa palepale na mmoja alijeruhiwa. Wanafunzi hao walikuwa upande wa kushoto wa barabara na eneo hilo lina utelezi kutokana na mvua iliyokuwa inanyesha,” alisema Maigwa.
Amesema polisi wanaendelea kumsaka dereva wa gari hilo ambaye alikimbia baada ya kuwagonga wanafunzi hao, kisha gari kupinduka.