The House of Favourite Newspapers

Sababu za mtu kushindwa kupunguza uzito

UKWELI ni kwamba kula kwa kuzingatia matakwa ya afya yaani kufanya dayati ni ngumu kwa baadhi ya watu kwa sababu kuna mambo mengi yanayochangia ugumu huo hivyo kubaki na unene wao; mambo hayo ni:

  • KUTOKUJUA AINA YA VYAKULA VINAVYOFAA

Wengi hushindwa kufanya dayati kwa muda mrefu kwani hajui chakula gani humfaa hivyo kuzidi kunenepa na kuzidisha uzito, matokeo yake wengi hushinda njaa au hula matunda na mboga tu na kujikuta mwili ukidhoofika.

  • GHARAMA YA VYAKULA HIVYO

Dayati nyingi huwa na ratiba ya kula pamoja na aina ya vyakula unavyotakiwa kula kwa kila mlo. Mara nyingi vyakula hivi huwa na gharama kubwa hivyo huongeza gharama katika familia na kufanya wengi washindwe dayati hizo.

  • NJAA KALI:

Dayati nyingi huelekeza mtu ale chakula kidogo sana na wakati mwingine vyakula hivi humfanya mtu kujisikia njaa kwa sababu hashibi, hivyo huwa na njaa kali na kuamua kula atakavyo, hivyo kuzidi kunenepa.

  • HAMU YA KULA VYAKULA WANAVYOKULA WENGINE

Harufu nzuri na muonekano wa chakula wanachokula wengine hapo nyumbani mara nyingi huleta hamu ya kula na pia huongeza njaa, hii hufanya wengi waharibu dayati zao kwa kula vyakula hivyo ambavyo si sehemu ya dayati zao na kuongeza uzito kwa kunenepa.

  • UGUMU WA KUACHA VYAKULA UNAVYOVIPENDA

Ni wazi kabisa kwamba ni ngumu sana kuacha kula vyakula unavyovipenda na ulivyovizoea. Ni ngumu zaidi kama kuna aina fulani ya chakula ambayo imekua kama kilevi kwako. Mfano kuna watu asipokunywa soda fulani au juisi fulani basi siku kwake haijaisha. Hufanya hivyo bila kuzingatia kwamba wanajiongezea uzito. Soda na vyakula vyenye sukari ni hatari sana kwa afya yako kwani huongeza unene.

  • KUVUNJWA MOYO NA WANAOKUZUN­GUKA

Mara nyingi watu wanaokuzunguka hukuvunja moyo kwa maneno yao, hasa pale unapofanya juhudi za kupunguza unene halafu wao wanakuambia huna mabadiliko hata kama umepungua. Wengine hukata tamaa na kuamua kula na kuendelea kunenepa.

Mbaya zaidi kama mhusika alikuwa anataka apate matokeo mazuri ya kupungua unene haraka, wengi wanataka kupunguza mzito mkubwa kwa muda mfupi jambo ambalo si rahisi.

  • UZITO MKUBWA

Uzito mkubwa sana unafanya mtu aone haiwezekani kupungua kwani inachukua muda mrefu kuona matokeo makubwa. Ni vyema kujua kuwa kila hatua ndogo unayochukua husaidia kupunguza unene na matokea huja hata kama yatachelewa, usikate tamaa.

  • KERO

Mara nyingi marafiki na ndugu huwa kero kwa maneno yao hasa pale wanapotaka kukuambia fanya nini na uache nini ili upungue unene.

Ni vyema kujua kwamba unapoona ndugu au rafiki ameamua kupunguza uzito basi ana sababu za kufanya hivyo na anajua ni nini faida yake, usimkatishe tamaa, mwache apungue unene kwa afya yake

Comments are closed.