The House of Favourite Newspapers

Sakata la Mwakalebela, TFF Giza Nene

0

LICHA ya kukutana na kufanya kikao kizito kati ya viongozi wa Klabu ya Yanga na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), lakini hatma ya kikao hicho haijawekwa wazi nini kinaendelea juu ya adhabu ya Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Frederick Mwakalebela.

 

Hiyo ikiwa siku chache tangu serikali iziagize pande mbili kukutana na kumaliza tofauti zao kisha kuwasilisha uamuzi wao kama mrejesho baada ya Yanga kulalamika wizarani kuonewa na TFF.

 

Klabu hiyo ilipeleka malalamiko hayo kwenye Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Serikali kuagiza pande hizo kukutana na kupata mwafaka.

 

Yanga walipeleka malalamiko hayo ikiwa ni wiki moja imepita tangu Mwakalebela afungiwe kwa muda wa miaka mitano sambamba na faini ya Sh 5m baada ya kukutwa na makosa mawili.

 

Juzi Jumatatu asubuhi viongozi wa Yanga wakiongozwa na Mwenyekiti Dk Mshindo Msolla walifi ka makao makuu ya shirikisho hilo na kufanya kikao ambacho serikali iliagiza kifanyike baina yao na TFF kumaliza sintofahamu inayojitokeza baina ya pande hizo.

 

Kikao hicho kilianza saa nne asubuhi na kumalizika majira ya saa nane mchana hadi wanatoka katika kikao hicho mchana, hakuna kiongozi wa Yanga wala TFF aliyekuwa tayari kuelezea kilichozungumzwa lakini ajenda kuu ilikuwa malalamiko ya Klabu ya Yanga kutotendewa haki na TFF katika masuala mbalimbali.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo gazeti hili imezipata, upo uwezekano mkubwa wa Mwakalebela kufunguliwa kifungo cha miaka mitano cha kutojihusisha na soka sambamba na kuondolewa faini hiyo.

 

Alipotafutwa Mwakalebela kuzungumzia hilo alisema: “Mimi sijapewa taarifa yoyote kuhusiana na kikao hicho, kwani sikuwepo sehemu ya viongozi wa Yanga waliohudhuria kikao hicho, kwani waliohudhuria ni katibu Mfi kirwa (Haji) na Mwenyekiti Msolla.”

STORI: WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam

Leave A Reply