The House of Favourite Newspapers

Sakho Afunika Balaa Simba SC

0

KIUNGO mshambuliaji mpya wa Simba, Pape Ousmane Sakho ambaye amerithi jezi namba 17 iliyokuwa ikivaliwa na kiungo fundi Mzambia, Clatous Chama ndiye mchezaji aliyefunika zaidi kwa kuwa na takwimu bora katika kipindi cha wiki tano za maandalizi ya kabla ya msimu ambayo yamefanywa na klabu hiyo.

Katika kambi zote mbili za kabla ya msimu, Simba ilicheza michezo mitano ya kirafiki ambapo walishinda michezo miwili, na kutoa sare kwenye michezo mitatu, huku Sakho akifanikiwa kufunga mabao matatu katika michezo hiyo mitano.

Sakho alifunga mabao mawili dhidi ya timu mbili za Morocco (Far Rabat na Olympique Club de Khouribga), huku bao moja akifunga kwenye ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Fountain Gate.

Simba ilikuwa na kambi mbili za kabla ya msimu ambapo kambi ya awamu ya kwanza ilifanyika kwa kipindi cha wiki tatu mwezi Agosti mwaka huu nchini Morocco, kabla ya kurejea nchini na kuweka kambi ya awamu ya pili jijini Arusha ambapo ilitarajiwa kumalizika jana Alhamisi.

Nyota huyo ambaye msimu uliopita alitwaa tuzo ya mchezaji bora wa Ligi Kuu ya Senegal alijiunga na kutangazwa rasmi na Simba Agosti 14, mwaka huu akitokea klabu ya Teungueth ya Senegal.

Akizungumzia maandalizi yao ya kabla ya msimu ‘Preseason’, Sakho alisema: “Nimefurahia maandalizi ya kikosi chetu, na kuwa sehemu ya watu walioipa matokeo timu kupitia kufunga mabao, nashukuru pia kwa juhudi za timu nzima. Naamini Mwenyezi Mungu atanisaidia na kupata nafasi ya kuifungia timu yangu magoli mengi zaidi.”

Joel Thomas, Dar es Salaam

Leave A Reply