The House of Favourite Newspapers

Sanchi mahari ya milioni 10 kwani umekuwa ng’ombe?

0
Modo mwenye figa bomba, Jane Ramoy ‘Sanchi’.  

JANE Rimoy, ni jina la msanii ambaye amejizolea umaarufu mkubwa katika viunga vya burudani Bongo baada ya kuonekana kufanya vizuri katika kupamba video vya wasanii wa Muziki wa Kizazi Kipya, au kama wenyewe tunavyosema, Bongo Fleva. Hata hivyo, mashabiki hao wanamfahamu zaidi kwa jina lake la Sanchoka au Sanchi!

 Umbo lake kubwa limemfanya kuwa kivutio, ingawa mara kadhaa wadau wamekuwa wakihoji uhalali wa mwili wake, wakihofu kuwa huenda anatumia madawa ya kuongeza ukubwa, ambapo hapa kwetu zinafahamika zaidi kama Mchina. 

Kabla ya kukutana naye ana kwa ana, hata mimi nilikuwa na hisia hizo, lakini nilipomtia machoni na kufanya naye mazungumzo kuhusu mwili wake, niliona kuwa ni mwili wake kweli. Binti amekaa vizuri. 
Kwa wanaume wadhaifu wa miili mikubwa ya akina mama hasa makalio, hapa wanapata presha. 

Kuna wakati mmoja, picha zake zilitembea katika mitandao mingi ikimuonyesha akichezesha makalio yake kwa namna ambayo haikuwa nzuri. 
 
Hiyo tisa, lakini hivi majuzi Sanchoka ametoa kauli ambayo imetembea sana huko mitandaoni na kwa vile hakujitokeza kukanusha, ni wazi ilikuwa ni yake na alidhamiria kupeleka ujumbe kwa mashabiki wake.

 Kuna kauli alisema mwanaume anayetaka kumuoa, basi ni lazima ajipinde na kutoa kiasi cha shilingi milioni kumi taslimu kama mahari yake! Ndiyo, shilingi milioni kumi kama mahari! Lakini hakuacha kufafanua, alisema anaona kiasi hicho anastahili ili kumfanya mwanaume atakayemuoa na kummiliki, atambue thamani yake, kwani wanawake wengi wamekuwa wakinyanyasika baada ya kuolewa kwa vile huolewa kwa mahari ndogo ambayo haifanani na wao.

 Ni kweli kwamba mwanamke anapaswa kujitambua thamani yake na hata kumweleza kwa maneno au hata kwa vitendo mwenza wake, lakini staili hii ya Sanchoka, kutaja kiwango cha fedha siyo sawa. Mahari ya milioni 10 kwani umekuwa ng’ombe? Kwanza nimwambie kuwa, utu hata siku moja haujawahi kuwa na kiwango cha fedha, yaani hakuna mkwanja wowote ambao unaweza kuthaminishwa na mtu! Watu wengi wanataja viwango vya fedha kama thamani zao kutegemea na nini wanafanya. 

Kwa mfano, kama Sanchoka atataka kupewa kiasi cha shilingi milioni tatu kwa mfano, ili atokee kwenye video ya msanii f’lani, ni sawa, kama ambavyo mwanasoka anavyotaka fedha za usajili kulingana na kiwango chake cha uchezaji uwanjani. 

Lakini mtoto wa kike unapotaja kiasi cha fedha ambacho mtu anayetaka kuwa mumeo inabidi atoe, inaleta ujumbe mwingine tofauti kabisa. Kwa namna ambavyo Sanchi amejitengeneza machoni mwa mashabiki, maneno aliyoyaandika yana tafsiri nyingi, lakini kwa namna alivyotaka watu waelewe, inaleta shida kidogo. 

Kama ni thamani ya utu wa mwanamke, haupatikani kwa kiwango cha fedha, kwa sababu kuna watu wana fedha, wanaweza kutoa na kumpatia, lakini kamwe asipate heshima ambayo yeye anadhani anayo. Na mwanaume hata siku moja hapati thamani ya mwanamke kwenye fedha, kwa sababu kama ni mtu anayependa fedha humtumia kama chombo cha starehe tu.

Mwanaume anayehitaji mwanamke wa kumweka ndani, huogopa sana kuchukua wanawake dizaini ya Sanchoka, kwa sababu wanaamini katika fedha. 

Maana, hata kama akipatikana bwana mwema anayeweza kuwa na msaada mkubwa kimaadili, hana nafasi kwa Sanchi kwa sababu tu hana kitu? Anaweza kupata wanaume wengi wenye kiasi hicho cha fedha, lakini kitu ambacho ninaweza kumhakikishia ni kuwa itamchukua miaka mingi sana kumpata mume bora wa ndoa. Watu watatoa pesa, ili wapate wanachovutiwa kutoka kwake halafu wataendelea na maisha mengine, siku atakayokuja kushtuka, umri ushamtupa mikono na hakuna tena mtu wa kumtamani kama mke.

NA OJUKU ABRAHAM | IJUMAA | BARUA NZITO

Leave A Reply