The House of Favourite Newspapers

Sasa Wanalalamika Simba, Baadaye Itakuwa Yanga

 

LIGI Kuu Tanzania Bara inaendelea tena leo Ijumaa kwa mechi kadhaa ambazo zinatarajiwa kupigwa kwenye vi­wanja mbalimbali.

 

Ni ligi ambayo imeleta minong’ono mingi sana kupitia kwa mashabiki, wengi wameshaanza kuzungumza mambo mengi, wen­gine wakiamini kuwa kuna utara­tibu mbovu sana kwenye ratiba ya ligi hiyo.

Baadhi ya watu akiwemo mse­maji wa Simba, Haji Manara wame­shaanza kutoa tahadhari juu ya kile ambacho kinatokea, hajasema moja kwa moja kuwa kuna kosa lakini ametumia mtandao wake wa kijamii kama vile kutoa tahadhari.

 

Ni kweli wengi wanaolalamika wapo sahihi kwa kuwa wanaona siyo sawa kwa timu moja kucheza michezo mingi nyumbani.

 

Yanga watacheza michezo 12 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, halafu baada ya hapo ndiyo watatoka nje ya Jiji la Dar es Salaam.

Tatizo hapa siyo Yanga, bali ni yale ambayo nilikuwa nasema siku zote kuwa kitendo cha kuwa na timu 20 kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara kina madhara yake.

 

Hii ni moja ya changamoto ya kuwa na timu 20 kwenye ligi, Yan­ga hawachezi Taifa michezo hiyo haina maana kwamba wanapen­delewa bali wanacheza hapo kwa kuwa timu nyingi hazina uwanja wa kutumia.

 

Kwa sasa zaidi ya timu tano kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara zi­takuwa zinatumia viwanja vyake Dar es Salaam na hivyo ni ligi ya ukanda mmoja.

Yanga, Simba, African Lyon, JKT Tanzania, Azam ni timu ambazo zipo Dar es Salaam na nyingi zina­tumia Uwanja wa Uhuru, Chamazi na ule wa Taifa jijini Dar es Salaam.

 

Haya ni matatizo kwa kuwa timu zote hizo hazina viwanja ndiyo maana inaonekana hali kama hiyo.

Kama African Lyon wangekuwa na uwanja wao Bagamoyo, Simba Chalinze na Yanga Mbande haya yote yasingetokea, lakini kwa kuwa TFF wanaruhusu hata uwanja am­bao wanadang’anywa ndiyo wa­natengeneza matatizo haya.

 

Shirikisho la Soka la Kimataifa ‘Fifa’ wakiuliza uwanja wa Simba upo wapi TFF wanawaonyesha Uwanja wa Taifa, wakiuliza Uwanja wa Yanga wanawaonyesha Taifa, Mtibwa Sugar, Taifa.

Nafikiri kama TFF wangekuwa makini kuhakikisha kuwa wanasi­mamia soka letu ipasavyo kila timu ingekuwa na uwanja.

 

Nimewahi kufuatilia kwa kipindi kifupi na kugundua kuwa TFF wa­nachangia kwa sehemu kubwa sana klabu zetu kutojenga vi­wanja kwa kuwa wanaonyesha kama siyo kitu muhimu kwenye soka.

Hii litakuwa tatizo kubwa kwetu kwa muda mrefu, na hali hii ndiyo inachangia soka letu linashindwa kukua kwa kasi inayotakiwa.

 

Kama TFF wakisimamia soka vizuri hakika haya yasingetokea, awali wakati wanaongeza timu kufikisha 20 wakati wa timu 16 bado nusu ya timu zilikuwa zime­jikusanya kwenye kanda moja jambo ambalo pia lilisababisha mechi nyingi kuchezwa sehemu ndogo.

 

Swali kubwa la kujiuliza ni kwamba mwishoni mwa msimu huu Yanga nao watalalamika kuwa Simba amemalizia mechi nyingi nyumbani kwa kuwa kama Yanga wanacheza hapo sasa la­kini ifahamike kuwa Simba nao watacheza hapo na idadi ya michezo inafanana.

 

Kwa sasa inazungumzwa ya Yanga kwa kuwa ndiyo ipo kwenye mzunguko wa kwanza lakini baadaye itazungumzwa ya Simba kwa kuwa nayo lazima itachezwa kwenye ligi hii.

Na haya yatakuwa malalamiko ya klabu na TFF kwa kila msimu hadi pale timu zitakapokuwa na viwanja vyao ambavyo zitakuwa zikivitumia.

Ni Mtazamo Wangu – PHILLIP NKINI

Comments are closed.