The House of Favourite Newspapers

Sasha Alia Kutishiwa Kuuawa!

Sasha Kassim

VIDEO Queen mwenye figa matata Bongo, Sasha Kassim amelazimika kukimbilia katika kituo cha polisi cha Mtongani jijini Dar akidai kuwa, mwanamke mmoja aliyemtaja kwa jina la Mama Aisha anatishia kumuua.

Akizungumza na gazeti hili, Sasha alisema kuwa, kuna wakati aliwahi kudaiwa kupora mume wa mama huyo na kuanzia kipindi hicho amekuwa akipokea vitisho vya hapa na pale.

“Huyu mama (mama Aisha) alipoachana na mumewe, akadai eti mimi ndiye nimemvunjia ndoa, nikashangaa sana lakini hivi karibuni nimepata taarifa kuwa anapanga kunimwagia tindikali. “Nilipata hofu sana lakini jamani labda leo niseme ukweli kwamba sikuwa na uhusiano na mume wa mama huyu, nilikuwa naenda pale nyumbani kwake maana dada yangu anaishi jirani.

“Yeye anashikilia kuwa mimi nilionekana nyumbani kwake kwenye kochi, ni kweli kabisa ila ulitokea msiba, nikawa naogopa kukaa kwa dada yangu, ndo’ nikaenda pale nyumbani kwa yule baba kama jirani tu lakini hakuna ishu ya mapenzi, aache kuniwazia mabaya kabisa,” alisema Sasha na kuongeza:

“Nimeona nisikae tu maana linaweza kunitokea lolote, nimeenda kufungua jalada kwenye kituo cha Polisi cha Mtongani lenye namba MT\ RB\1477\2018 KUTISHIA KUUA KWA MANENO.” Kufuatia malalamiko hayo ya Sasha, mwandishi wetu alimtafuta Mama Aisha kupitia simu yake ya mkononi na alipopatikana alifunguka hivi:

“Jamani huyo Sasha amejikosha kwani alichokifanya anakijua yeye, mimi sijawahi kusema kwa mtu eti nitamwagia tindikali.” Hivi karibuni Mama Aisha alimtuhumu Sasha kumpora mume wake na kudai kuwa ndiye aliyesababisha ndoa yake kuvunjika.

STORI: Waandishi Wetu, Risasi Mchanganyiko

Comments are closed.