SHIRIKA la Utangazaji la Marekani, Voice Of America (VoA) limeitembelea Televisheni ya Mtandaoni, Global TV Online katika ofisi zake zilizopo Sinza Mori jijini Dar es Salaam na kufanya mazungumzo na wafanyakazi wa Televisheni hiyo kwa lengo la kupanua wigo wa utendaji kazi ya kuupasha umma habari kote duniani.
Akizungumza mara baada ya kuwasili Global TV Online, Mkuu wa Idhaa ya Kiswahili ya VoA, Mwamoyo Hamza amesema amefurahishwa na uhusiano mzuri uliopo kati ya Global TV Online na VoA wa kuupasha habari umma wa Watanzania na dunia nzima huku akisisitiza kuendeleza kuumarisha ushirikiano huo ambao utakuwa na tija kwa taifa na walimwengu wengine.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Makampuni ya Global Group ambayo pia yanamiliki Global TV, amesema anajivunia ushirikiano huo huku akiahidi kushikama na VoA kwa kubadilishana habari, kutoa habari zenye weledi na tija kwa umma na taifa zima.
Aidha, Shigongo amesema Global TV Online ambayo ni Televisheni inayoongoza kwa ubora na kufuatiliwa na watu wengi zaidi nchini, itaendelea kutoa habari zilizo bora kwa kuzingatia sheria za nchi, maadili na kanuni za tasnia ya habari.
Kwa sasa Global TV Online na mtandao wa www.globalpublishers.co.tz vimekuwa vikishirikiana na VoA kwa miaka mingi ikiwa ni pamoja na habari, matukio, picha na video zinazopatika kwenye mitandao hiyo ambazo zimekuwa zikitumiwa na VoA, na habari zinazorushwa na VoA zimekuwa zikitumiwa pia na Global TV Online na www.globalpublishers.co.tz.
Pia kuna vipindi na taarifa za habari (Duniani Leo, kila siku jioni) kutoka VoA ambavyo vimekuwa vikirushwa kupitia Global TV Online ikiwemo; Washington Bureau, kinachotangazwa na Sunday Shomari kila Jumanne saa 5:00 asubuhi, Shaka Extra Time cha Shaka Ssali kila Jumatano saa 5:00 asubuhi na Straight Talk of Africa cha Shaka Ssali, kila Alhamisi saa 5:00 asubuhi.
Na Musa Mateja/Global TV Online.
Comments are closed.