The House of Favourite Newspapers

Serikali Kugharamia Mazishi ya Mwanafunzi wa NIT, Akwilina (Video)

Waziri wa Elimu, Profesa. Joyce Ndalichako amesema kuwa serikali itagharamia shughuli za mazishi ya Mwanafunzi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Akwiilina Akwilina ambaye ameuawa kwa kupigwa risasi Februari 16, 2018 eneo la Mkwajuni DSM.

Mwanafunzi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Akwiilina Akwilina enzi za uhai wake.

Waziri Ndalichako amesema kuwa viongozi mbalimbali wameguswa na kifo hicho kwani mwanafunzi huyo hakuwa na hatia yoyote na kusema kifo chake ni pigo kubwa kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Marehemu Akwilina alikua ni miongoni mwa wanaufaika wa mikopo ya elimu ya juu, wizara yangu itamkumbuka marehemu Akwilina kama mmoja ya wanafunzi wa kike ambao wamejipambanua katika kutambua na kuthamini umuhimu wa elimu na hivyo kuwa katika mstari wa mbele kuhakikisha anasoma kwa bidii kwa manufaa yake mwenyewe, familia yake na manufaa mapana ya taifa letu kwa ujumla”

Ndalichako amedai kuwa kifo cha mwanafunzi huyo kimetokea wakati akiwa kwenye harakati ya kupeleka barua ya maombi ya mafunzo kwa vitendo ambayo alikuwa akitegemewa kuanza Februari 26, 2018 na kudai kifo hicho kimezima ndoto yake na serikali kukipokea kwa masikitiko.

“Mimi Waziri mwenye dhamani ya elimu nimesikitika sana kuona binti huyo amepoteza maisha akiwa katika kutekeleza shughuli zake za kielimu, Wizara yangu itagharamia mazishi ya marehemu Akwilina hadi hapo atakapopumzishwa katika makao yake ya milele, namuagiza Katibu wangu kuakikisha kwa pamoja tunasimamia shughuli zote za msiba huu”

Aidha Waziri waliviomba vyombo vya usalama kufanya uchunguzi kwa haraka ili kuwatambua na kuwakamata watu ambao wamesababisha kifo cha mwanafunzi huyo ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yao.

Comments are closed.