Serikali Ya Tanzania Yaingia Makubaliano Na Klabu Ya Seattle Sounders Ya Marekani
SERIKALI ya Tanzania imeingia makubaliano klabu ya Seattle Sounders inayocheza Ligi Kuu ya mpira wa miguu ya Major (MLS) Seattle Seahawks inayocheza ligi ya taifa (NFL) na timu ya mpira wa kikapu ya Portland Trailblazers inayocheza Ligi ya NBA ili kutangaza utalii na uwekezaji nchini.
Timu hizo ambazo zipo chini ya taasisi ya Vulcan Inc zinamilikiwa na Paul Allen mwanzilishe mwenza wa Microsoft ziliingia makubaliano na serikali ya Tanzania jana Mei 5, 2023 katika uwanja wa Lumen nchini Marekani ambapo kwa Tanzania iliwakilishwa na Katibu Mkuu Wizara ya Mali Asili na utalii Dk Hassan Abbas na Mkurugenzi wa Bodi ya utalii nchini (TTB) Damas Mfugale.
Akizungumza mara baada ya kusaini makubaliano hayo katika hafla fupi iliyoandaliwa na kampuni ya Vulcan na kushirikisha wadau kutoka makampuni mbalimbali yaliyoko jijini Seattle ikiwemo wawakilishi kutoka Google, Starbucks, ofisi ya Meya wa Seattle, Boeing na jumuiya ya wafanyabiashara Katibu Mkuu wa Wizara ya Mali Asili na Utalii, Dk Hassan Abbas amesema serikali ya Tanzania imedhamiria kwa dhati kuongeza juhudi za kutangaza utalii kupitia michezo pia kushirikiana na taasisi mbalimbali duniani ili kuongeza idadi ya watalii kutoka nje ili kuongeza mapato zaidi kwa Serikali.
Naye, Mmiliki wa klabu hizo Adrian Hanauer amesema ni jambo jema kuingia makubaliano na Tanzania, anaifahamu Tanzania ni nchi nzuri na kuwataka wafanyabiashara wa Marekani ambao hawajawahi kufika nchin waje kutembelea na kuwekeza Tanzania.
“Nimewahi kufika Tanzania, naweza kuwahakikishia kuwa kwa wale ambao hawajafika mfike ni nchi nzuri sana. Tuliwahi kwenda pia Sounders miaka ya 2000 ikacheza na Yanga, Simba na Timu ya Taifa,”amesema Adrian Hanauer, ambaye kwa sasa ni mmiliki mwenye hisa nyingi wa klabu ya Seattle Sounders akiahidi klabu hiyo na wadau wengine wako tayari kushirikiana kusukuma mbele utalii wa Tanzania.