The House of Favourite Newspapers

SERIKALI YAFUNGUKIA WALIOSAMBAZA VIDEO YA ULAWITI YA AMBER RUTTY

GUMZO kubwa mtaani kwa sasa ni juu ya kesi inayomkabili mwanamuziki Ruth Abubakar ‘Amber Rutty’ ambaye video yake imevuja ikimuonesha akifanyiwa ulawiti na mwanaume na sasa serikali kupitia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania, TCRA imefungukia hofu waliyo nayo baadhi ya watu ambao walipopokea video hiyo kwenye simu zao, waliwatumia wenzao.  Awali yalikuwepo maelezo kuwa, endapo mtu atatumiwa kitu ambacho kipo kunyume na maadili ya Kitanzania kisha akamtumia mtu mwingine, anaweza kutiwa hatiani na kushtakiwa lakini kumbe kwa hili la Amber Rutty ni tofauti kidogo.

BAADA YA VIDEO KUVUJA

Mara baada ya kuvuja kwa video hiyo ikimuonesha msanii huyo akifanyiwa mchezo mchafu na mwanaume ambaye haonekani, vijana wa mjini walianza kutumiana kupitia simu zao za kisasa ‘smart phone’ huku wengine wakizifuta haraka kwa kuogopa sheria kuwabana.

“Daah! Hivi umeiona video ya Amber Rutty? Aisee ni mbaya sana, yaani mimi ilipoingia kwenye simu yangu tu nikafuta wala sikumtumia mtu maana si unajua mambo ya sheria,” alisikika akisema Jafari Juma, kijana anayefanya biashara ya kuuza simu Kariakoo jijini Dar. Mwingine ambaye ni mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Azania jijini Dar, Fred Kizoa alisema kuwa, mara baada ya kuona video hiyo alijaribu kuwakumbusha wenzake kuwa, kumtumia mtu mwingine ni kosa hivyo ni vyema kila anayetumiwa akaifuta.

“Unajua watu hawajui madhara ya kutumiana vitu kama hivi, hawajui kwamba mbali na yule aliyejirekodi kisha kusambaza, hata anayetumiwa kisha kumtumia mwingine na mwingine anaweza kuchukuliwa hatua. “Kwa kifupi jamii yetu imeoza. Yaani vijana wanaona sifa kuwa na video kama zile kwenye simu zao, jambo ambalo linaipeleka jamii yetu kubaya,” alisema mwanafunzi huyo.

TCRA WAFUNGUKIA WALIOTUMIANA VIDEO HIYO

Kufuatia hofu hiyo iliyotanda mtaani ya wananchi wengi kuogopa kuhifadhi video chafu za msanii huyo wala ‘kufowadi’ kwa mwingine, mwandishi wetu alifanya jitihada za kuzungumza na Mamlaka ya Mawasiliano, TCRA ambapo mmoja wa maofisa aliyeomba jina lake lisitajwe gazetini kwa kuwa siyo mzungumzaji rasmi alisema kuwa, sheria kwenye sakata la video ya Amber Rutty linamgusa moja kwa moja mhusika kwa kuwa imebainika yeye ndiye aliyejirekodi kisha kusambaza mwenyewe.

“Kwenye hili aliyejirekodi video chafu kisha kuisambaza mwenyewe, ndiye ambaye sheria inadili naye. Wale ambao wanatumiana sheria inaweza isiwahusu,” alisema afisa huyo. Akimzungumzia mwanaume ambaye haonekani kwenye video hiyo ya Amber, ofisa huyo alisema: “Sheria inambana mwanamke na yule mwanaume anayemfanyia ule mchezo, kwa maana hiyo akipatikana na yeye lazima sheria impitie.”

Mbali na ofisa huyo kutoa maelezo hayo kuhusu wale walitumiana video chafu ya msanii huyo, mwanasheria mmoja ambaye aliomba jina lake lisiandikwe gazetini alisema: “Ni kweli kwenye tukio kama hili la Amber Rutty, sheria inaweza kumbana yule aliyejirekodi na kuisambaza lakini sasa, kuna kipengele ambacho kinaweza kuwabana pia wale ambao wanatumiana vitu vichafu.

“Ndiyo maana inashauriwa kuwa, ili kuwa salama, unapopokea video chafu kama ya Amber, unaifuta. Kitendo cha wewe kuihifadhi kwenye simu yako kwanza ni kinyume na sheria lakini kumtumia mwingine ni jambo linaloweza kukuingiza matatizoni. “Kwa hiyo ushauri wangu mimi ni kwamba, hii tabia ya kupenda kutumiwa na kutuma picha chafu, haikubaliki kwenye jamii. Wanaofanya wanakiuka maadili na wewe unayefurahia na kusambaza uchafu huo unazidi kuyaharibu maadili, kwa kifupi ukipokea video yoyote mbaya, futa, kisha kaa kimya,” alisema mwanasheria huyo.

TUKIO LA AMBER RUTTY

Hivi karibuni msanii huyo ambaye hana umaarufu kivile aliachia video ikimuonesha akifanya mapenzi kinyume na maumbile na mwanaume ambaye haonekani.

Baada ya video hiyo kuvuja, Amber Rutty alijitokeza hadharani na kuomba msamaha lakini watu walimpuuza hasa baada ya kubainika kuwa, alifanya vile ili kutafuta kiki. Kufuatia kuchafuka kwa hali ya hewa kutokana na video hiyo kusambaa kama moto wa kifuu, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kupitia ukurasa wake wa Instagram alimtaka mwanadada huyo kwenda mwenyewe kujisalimisha kwenye kituo chochote cha polisi.

Mbali na maeleo hayo ya Makonda, Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola naye alikopi maeleo hayo kisha kuyapesti kwenye ukurasa wake wa Instagram, kuonesha kuwa anaungana naye. Kufuatia kukomaliwa huko, Amber Rutty juzi Ijumaa aliripoti kwenye Kituo cha Maturubai kilichopo Mbagala jijini Dar.

Taarifa iliyolifikia gazeti hili wakati likienda mtamboni inaeleza kuwa, taratibu za kumfikisha mwanadada huyo mbele ya sheria zinaendelea ili iweze kuwa fundisho kwa wengine. Ama kweli serikali kwenye kusimamia maadili haipoi mpaka kieleweke!

Comments are closed.