The House of Favourite Newspapers

Seven Days in Hell (Siku Saba Kuzimu)- 19

0

ILIPOISHIA:

Kuna wakati hofu ilinizidi na kutaka nigeuze nilikotoka lakini kitu ndani ya moyo wangu kikaniambia nizidi kusonga mbele. Kadiri nilivyokuwa nazidi kusonga mbele ndivyo zile sauti zilivyokuwa zinazidi kuongezeka, nikazidi kutetemeka kwa hofu huku nikiwa sijui nini itakuwa hatma yangu.

SASA ENDELEA…

Sauti zilizidi kuongezeka, nikawa nasikia sauti nyingine zikiugulia maumivu makali mno, nilitamani nione nini kilichokuwa kinaendelea lakini sikuweza kutokana na lile giza. Ilifika mahali ikabidi niwe natembea kwa uangalifu sana kwani nilihisi nilikuwa nikipita jirani kabisa na wale watu waliokuwa wakilia kwa maumivu makali.

Kiasili mimi ni mwoga sana kiasi kwamba nikiwa nyumbani kwangu, hata panya akipita darini kwa kasi, lazima nitashtuka sana lakini nashangaa siku hiyo kadiri muda ulivyokuwa unasonga mbele ndivyo hofu ilivyokuwa inazidi kupungua.

Haikuwa rahisi kupita sehemu ambayo unasikia kabisa wenzako wanalia kwa kusaga meno kwa maumivu makali kama ile. Ukiachilia mbali sauti hizo za watu, kulikuwa pia na sauti za watoto wachanga waliokuwa wamepamba moto kulia, ungeweza kudhani wamelazwa kwenye siafu.

*Usikose kutembelea Simulizi za Majonzi

Nilizidi kutembea kusonga mbele kufuata ile sauti iliyokuwa ikiliita jina langu, zile sauti za watu zikaanza kupungua kidogo kuonesha kwamba tayari nilishapita eneo walilokuwepo, zikawa zinasikika za wale watoto wachanga huku pia sauti za wanyama wakali nazo zikianza kuongezeka.

Nikiwa naendelea kutembea, nilishtukia sauti ya kutisha ya ndege mkubwa ikija kwa kasi pale nilipokuwepo, kufumba na kufumbua nilijikuta nikipigwa kikumbo na ndege yule mkubwa ambaye hata sikuweza kujua ni ndege gani kutokana na jinsi alivyokuwa mkubwa.

Kucha zake kali zikaniparua upande wa shavu langu la kushoto na kunifanya nijihisi maumivu makali sana. Hata hivyo, nilijikaza na kuendelea kusonga mbele. Lile dege ambalo baada ya kunipiga kikumbo lilipotelea mbali, nililisikia likianza kurudi tena, safari hii likipiga kelele kwa sauti kubwa kuliko mwanzo.

Sikumbuki kama katika maisha yangu ya kawaida nimewahi kusikia mlio wa namna hiyo wa ndege. Ilibidi niwe makini lisije kuniumiza tena, nikainua mikono na kujiziba upande wa usoni, likaja kwa kasi na kunipita, nikasikia upepo ukinipuliza kisha likatokomea kule ile sauti iliyokuwa ikiniita ilikokuwa inatokea.

*Usikose kutembelea Simulizi za Majonzi

Nilipojigeuza pale lilipokuwa limeniparua, niligundua kwamba vitu vya majimaji vilikuwa vikinitoka. Niliamini kwamba ni damu kwa sababu binadamu anapoumia, kinachotoka ni damu ingawa kutokana na giza lile, sikuweza kuthibitisha hilo zaidi ya kuendelea kujiaminisha mwenyewe.

Nikiwa nazidi kuelekea kule ile sauti ilikotokea, kwa mbali nilianza kuona kama mwanga hafifu ukionekana mita nyingi kutoka pale nilipokuwa nimefika. Nilishusha pumzi ndefu kwa sababu niliamini mwanga ni dalili ya uhai, nikajua lazima naweza kupata msaada nikifika pale kwani mpaka muda huo, sikuwa naelewa nini itakuwa hatima yangu.

Milio ya wanyama wa kutisha ilizidi kusikika kutoka kila upande lakini sikukata tamaa, nilizidi kusonga mbele huku giza bado likiwa nene vilevile, akili zangu zote zikiwa ni kwenye ule mwanga niliokuwa nauona. Cha ajabu, licha ya kutembea sana, bado ule mwanga uliendelea kuonekana ukiwa umbali uleule, jambo ambalo lilinishangaza sana.

Nilijaribu kuongeza urefu wa hatua lakini ilikuwa sawa na kazi bure, miungurumo ya wanyama wakali ikawa inazidi kuongezeka huku kwa mbali nikisikia sauti kama za yule ndege mkubwa aliyenijeruhi zikija tena lakini tofauti na awali, safari hii ilionesha kwamba walikuwa zaidi ya mmoja kutokana na ukubwa wa sauti zao.

“Mungu wangu, nimekwisha,” nilijikuta nikijisemea moyoni lakini jambo la ajabu tena, wakati mimi nikiamini maneno hayo niliyasemea moyoni, yalisikika kwa sauti kubwa utafikiri nimezungumza kwa kufumbua mdomo.

“Jamal mbona hufiki? Fanya haraka,” ile sauti iliyoniita ilisikika tena kutokea umbali ambao siwezi kuukadiria, nikataka nifumbue mdomo na kumuuliza yule mtu aliyekuwa ananiita ni nani, pale ni wapi na nilipelekwa pale kufanya nini lakini nilipofumbua mdomo, nilishangaa sauti ikiwa haitoki.

“Leo ndiyo mwisho wa maisha yangu,” nilijisemea moyoni baada ya kuona nimeshindwa kuwasiliana na yule mtu lakini cha ajabu tena, sauti ilisikika kwa nguvu. Nilishangaa sana, yaani nikifumbua mdomo na kuzungumza, sauti haisikiki lakini nikizungumza kimoyomoyo ndiyo sauti inasikika, nilibaki nimepigwa na butwaa.

Niliamua kujaribu kitu, kuzungumza kimoyomoyo kumuuliza yule mtu yale niliyotaka kumuuliza. Cha ajabu sasa, sauti yangu ndiyo ilisikika kwa nguvu na naamini yule mtu aliyekuwa ananipa maelekezo alinisikia.

*Usikose kutembelea Simulizi za Majonzi

“Wewe ni nani? Hapa ni wapi na kwa nini nimeletwa huku?”

“Mh! Hutakiwi kuuliza swali lolote,” ilisikika sauti ile kwa mwangwi mkubwa kama ilivyokuwa mwanzo.

“Mbona natembea lakini sifiki?” nilijisemea tena moyoni lakini sauti ikasikika vizuri kabisa.

“Geuka ulikotoka,” ilisikika ile sauti, safari hii milio ya wale ndege wakubwa ilikuwa imekaribia kabisa na kwa jinsi walivyokuwa wanakuja kwa kasi, nilijua lazima watanijeruhi tena.

Nilijaribu kugeuka kwa kutumia upande wa kulia lakini nikashangaa mwili wangu ukiwa mzito mno, nikajaribu upande wa kushoto, nikageuka bila tatizo lolote, nikawa natazama kule nilikotokea ambako nako kulikuwa na giza totoro kama kule nilikokuwa naelekea, tofauti yake ni kwamba huku nilikogeukia hakukuwa na mwanga unaoonekana kwa mbali.

“Haya tembea kinyumenyume,” ilisikika ile sauti, kweli nilipojaribu kupiga hatua moja tu, nilijikuta mwili ukiwa mwepesi sana, nikawa naenda bila kikwazo chochote, huku nyuma sauti za wale ndege zikawa zinazidi kufifia. Ndani ya muda mfupi tu, tayari nilikuwa nimefika pale ule mwanga ulipokuwa unatokea, niliisikia ile sauti ikiniamuru kugeuka, nikafanya hivyo, macho yangu yakatua kwenye jiwe la ukubwa wa wastani lililokuwa likiwaka bila kuteketea.

Nilishangaa sana kuona jiwe likiwaka, tena moto mkali unaoweza hata kuchemsha maji ndani ya muda mfupi. Hata hivyo, licha ya kwamba jiwe hilo lilikuwa likiwaka, mwanga wake haukuweza kunisaidia kuona chochote, nikawa naangaza macho huku na kule nikitarajia naweza kumuona yule mtu aliyekuwa ananipa maelekezo lakini haikuwa hivyo.

Kufumba na kufumbua, lile jiwe lilianza kutetemeka kama kuna tetemeko la ardhi kisha likaanza kubingirika kuelekea upande wa kushoto kutoka pale lilipokuwepo. Nilishtuka mno, nikawa natetemeka kwa hofu kubwa. Likaendelea kubingirika kwa kasi huku ikionesha kwamba kule lilikokuwa likiendelea kulikuwa na mteremko.

Sijui akili gani ilinituma kuanza kulifuata lile jiwe kwani hakika huo haukuwa uamuzi sahihi. Nilipopiga tu hatua moja, nilijikuta nikianza kuserereka kuelekea kule lile jiwe lilikokuwa linaelekea.

Nilijaribu kufunga breki lakini ilikuwa sawa na kazi bure, niliendelea kuserereka na kila nilipojaribu kujishikiza sehemu, sikuona chochote cha kunisapoti, ikafika mahali na mimi nikawa nabingirika kulifuata lile jiwe huku mteremko ukizidi kuwa mkali kadiri nilivyokuwa nasonga mbele.

Kwa mbali nilianza kuhisi joto kali huku lile giza nene likianza kupungua na kumezwa na mwanga mwekundu ambao hata bila kuuliza, nilijua kuwa ni wa moto mkubwa uliokuwa unawaka. Zile sauti za watu waliokuwa wakilia kwa maumivu makali, nilianza kuzisikia tena lakini tofauti na awali, safari hii zilikuwa kubwa zaidi huku ikionesha kwamba zilikuwa zikitoka kwa kundi kubwa la watu.

Nilizidi kuserereka kwa kasi kubwa kuelekea kule chini huku joto nalo likizidi kuongezeka. Nikiwa mdogo nimewahi kusikia kwamba Jehanum kuna moto mkali unaowaka muda wote, ambao ni maalum kwa ajili ya kuwateketeza watu wanaofanya dhambi duniani.

*Usikose kutembelea Simulizi za Majonzi

Nilianza kuhisi kwamba huenda kule nilikokuwa nikisererekea ni kwenye moto wa Jehanum na zile sauti za watu waliokuwa wakilia kwa kusaga meno walikuwa ni watu wenye dhambi, nikajikuta nikitetemeka kuliko kawaida.

Mpaka muda huo nilikuwa nimeshindwa kabisa kujizuia nisiendelee kuporomokea kule chini, kwa mbali nikaanza kuliona shimo kubwa ambalo ukubwa wake hata sijui nifananishe na nini lakini kwa kifupi lilikuwa kubwa mno, lisilo na mwisho, moto mkali ukiwa unawaka ndani yake. Kibaya zaidi, na mimi nilikuwa nikiendelea kuporomoka kuelekea ndani ya shimo hilo, nikajua huo ndiyo mwisho wangu.

Je, nini kitafuatia? Usikose next issue au bofya Simulizi za Majonzi.

Leave A Reply